JUMATATU WIKI YA 19 YA MWAKA-B
10/8/2015
Somo: 2Kor 9:6-10
Zab: 111
Injili: Yoh 12:24-26
Nukuu:
“Lakini nasema neno
hili, Apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu,”
2Kor 9:6
“Kila mtu na atende kama
alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu
humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu,” 2Kor 9:7
“Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika
nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi,” Yoh
12:24
“Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye
nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele,” Yoh 12:25
TAFAKARI: “Unaweza kutoa bila
kupenda, ila huwezi kupenda bila kutoa.”
Wapendwa wana wa Mungu,
tunapotembea mabarabarani, tuwapo maofisini, tuwapo majumbani mwetu, tuwapo
sehemu za starehe kama kwenye mahoteli na mabaa, tunakutana na omba omba wengi
sana na kutokana na kero zao za kutuomba tunajikuta mara nyingi tunatoa bila
kupenda. Tunafanya hivyo ili tuondokana na kero ile. Endapo tunafanya jambo
hili kwa mtazamo huu, ni sawa na kupanda haba na matokea yake tutavuna hapa. Ni
tendo la utoaji lisilo na neema ya Mungu ndani yake. Kwa upande mwingine
tunapopenda kweli basi hatuachi kutoa.
Furaha ni kama kikohozi
huwezi kukizuia. Upatwapo na kikohozi itakulazimu kukohoa tu. Tendo hili ni
sawa na pendo la kweli. Pendo la kweli litakulazimu kutoa bila kujibakiza. Huku
ndiko kule kupanda kwa ukarimu kunakotupelekea kuvuna kwa ukarimu. Hivyo Mtume
Paulo anasema, “Apandaye haba atavuna
haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu,” 2Kor 9:6. Kupata neema na baraka za Mungu, ni kulitenda jambo
hilo pasipo kulazimishwa na wala si kwa huzuni. Tunafanya kwa upendo wa kweli
tukimtazama Yesu Kristo kama kielelezo chetu. Hivyo, “kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa
huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa
ukunjufu,” 2Kor 9:7. Je, mtazamo wako
wa utoaji upoje?
Injili ya
leo inatuzamisha zaidi katika tendo hili la kujitoa kwa ajili ya wengine.
Ukweli ni kwamba huwezi kujitoa bila kujibakiza ukabaki katika hali ile ile.
Tendo hili la kujitoa bila kujibakiza linatubadili mwono wetu na mfumo mzima wa
maisha. Je, Yesu ana maana gani anaposema, “Chembe
ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali
ikifa, hutoa mazao mengi,” Yoh 12:24. Ndugu yangu, ni katika kufa tunapata
uzima, na, ni katika uzima yatupasa kufa ili uzima ule uendelee siku kwa siku
na milele yote. Fumbo hili na mfano huu wa chembe ya ngano Yesu anautoa
akionyesha ni kwa mauti gani ataufia ulimwengu ili kuupa uzima wa milele hasa
kwa wale wanaomwamini. Vile vile kwa fumbo hili na mfano huu wa chembe ya ngano
Yesu anatutaka tuwe mfano kwa maisha tunayoishi kadiri ya wito wa kila mmoja
wetu.
Wapendwa tukichukulia maisha ya familia, Baba huleta uzima
katika familia yake anapojitoa kabisa na bila kujibakiza. Kwa kufanya hivi mke
wake anaongezeka na watoto pia. Ni kwa namna hiyo hiyo Mama katika familia
anapojitoa kabisa na bila kujibakiza analeta uzima katika familia yake kwa Mume
wake kuongezeka na watoto pia. Kwa upande wa watoto huleta uzima katika familia
kwa kutimiza nyajibu zao, mfano, kusoma vizuri na kwa bidii na kutumia
rasilimali fedha vizuri ili kesho wawe furaha na matumaini kwa wazazi wao.
Mfumo wa maisha haya ni sawa na mshumaa unaotoa mwanga huku ukifa kwa kuyeyuka.
Nami kama Mtawa na Padre, yanipasa kufa kila siku ili pale nilipo pawe na uhai
wa kweli. Nakufa kila siku kwa kutimiza wajibu wangu vyema. Huku ni kuichukia nafsi
yako kwa ajili ya uzima wako na wale walio wako na chini yako. Hivyo Yesu
anasema, “Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye
aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele,”
Yoh 12:25. Je, maisha yako na majitoleo yako yanamatokeo ya uzima wa milele?
Tumsifu Yesu Kristo!
EE YESU NIJALIE NEEMA YA KUJITOA BILA KUJIBAKIZA. AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario