JUMAMOSI WIKI YA 18 YA MWAKA-B
8/8/2015
Somo: Kum 6:4-13
Zab: 17:2-4, 47, 51
Injili: Mt 17:14-20
Nukuu:
“Sikiza, Ee Israeli; Bwana,
Mungu wetu, Bwana ndiye mmoja. Nawe
mpende Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa
nguvu zako zote,” Kum 6:4-5
“ndipo ujitunze, usije
ukamsahau Bwana aliyekutoa nchi ya Misri, nyumba ya utumwa,” Kum 6:12
“Mche Bwana, Mungu
wako; ndiye utakayemtumikia, na kuapa kwa jina lake,” Kum 6:13
“Bwana, umrehemu
mwanangu, kwa kuwa ana kifafa, na kuteswa vibaya; maana mara nyingi huanguka
motoni, na mara nyingi majini. Nikamleta
kwa wanafunzi wako, wasiweze kumponya,” Mt 17:15-16
“Yesu akajibu,
akasema, Enyi kizazi kisichoamini, kilichopotoka, nitakaa pamoja nanyi hata
lini? Nitachukuliana nanyi hata lini? Mleteni huku kwangu,” Mt 17:17
“Yesu akawaambia, Kwa
sababu ya upungufu wa imani yenu. Kwa maana, amin, nawaambia, Mkiwa na imani
kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa uende kule; nao
utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu,” Mt 17:20
TAFAKARI: “Mwamini Yesu pasipo
shaka nawe upate uponyaji.”
Wapendwa wana wa Mungu, “basi kwa imani ni kuwa na hakika
ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana,” Ebr 11:1. Kwa Imani
wana wa Israeli walimtumainia Mungu pale walipotengemea msaada wake na hata
pale walipokosa mwelekeo. Ni kwa Imani hiyo na uwezo wake Mungu juu ya historia
nzima ya wokovu wetu, Wayahudi wanathubutu kusema pasipo shaka: “Sikiza, Ee Israeli; Bwana, Mungu wetu, Bwana ndiye mmoja. Nawe mpende Bwana, Mungu wako, kwa
moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote,” Kum 6:4-5.
Maneno hayo yanabeba muhimili wote wa maisha yao, na historia nzima ya Taifa
hili la Waisraeli. Sala hii imebeba shukrani zote walizotendewa na Mungu tangu
mwanzo wa Taifa hili, na wanazidi kumwomba Mungu kudumisha uhusiano huu hadi
mwisho wa nyakati.
Kama
ilivyo historia hii ya Taifa hili la kiyahudi, hawakuweza kusahau mkono wa
Mungu kuwatoa utumwani Misri. Msingi huu wa Imani unarizishwa kwa vizazi vyote,
na kutaarifiwa hivi; “ndipo ujitunze, usije ukamsahau Bwana aliyekutoa nchi ya Misri,
nyumba ya utumwa,” Kum 6:12. Je, leo wewe
kama mzazi unawarizisha nini watoto wako? Mungu wetu anayetuwezesha kila kitu
katika maisha yetu ndiye tunayepaswa kumcha na kumtumikia. Hivyo, “Mche Bwana, Mungu wako; ndiye utakayemtumikia, na kuapa kwa jina
lake,” Kum 6:13. Je, ni jambo gani linalosukuma maisha yako? Wengi wetu
tunasukumwa na vyeo vyetu, nafasi zetu, mali na utajiri wetu, sifa na majigambo
yetu. Hivi vyote ni vizuizi vya kuuona uso wa Mungu. Yote tuliyo katika jamii
yetu leo na sasa yawe dhamana na njia ya kumjua Mungu, kumpenda, tumtumikie na
mwisho turudi kwake mbinguni kwenye umilele.
Imani
katika maisha ni jambo la msingi sana. Bila Imani hatuwezi kuishi hata chembe
ya uhalisia wa vitu. Ni kwa imani tunajibidisha kusoma na hata kufanya kazi kwa
bidii tukiwa na hakika ya mambo yatarawajiwayo. Hivyo hatupaswi kuwa na
mashaka, na hasa tukiwa na jemedari wetu mkuu Yesu Kristo. Mama mwenye shida na
ugonjwa wa mwanaye anamwendea Yesu kwa mashaka, na kusema, “Bwana, umrehemu mwanangu, kwa kuwa ana kifafa, na kuteswa
vibaya; maana mara nyingi huanguka motoni, na mara nyingi majini. Nikamleta
kwa wanafunzi wako, wasiweze kumponya,” Mt 17:15-16. Mama huyu anataka ishara
pasipo kuwa na Imani ya kutosha. Miujiza siyo msingi wa Imani, bali hukomaza
Imani. Jambo la msingi ni kuamini kwanza pasipo shaka. Kwa tendo hili la kuwa
na shaka katika Imani, Yesu anatoa angalisho: “Enyi kizazi kisichoamini,
kilichopotoka, nitakaa pamoja nanyi hata lini? Nitachukuliana nanyi hata lini?
Mleteni huku kwangu,” Mt 17:17. Yesu anajua kwa uhakika ipo siku hatutakuwa
naye kimwili, na hivyo tuwaamini wale aliowaweka wakfu kwa kazi yake, na hasa
Kanisa. Ni kwa Imani kila mbatizwa anaweza kufanya kazi azifanyazo Kristo.
Wanafunzi
wa Yesu wanakiri hawakuweza kufanya aliyoyafanya Yesu. Hivyo Yesu anawapa sababu
ya kutokufikia lengo lile na matamanio yao. “Yesu akawaambia, Kwa
sababu ya upungufu wa imani yenu. Kwa maana, amin, nawaambia, Mkiwa na imani
kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa uende kule; nao
utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu,” Mt 17:20. Je,
wamwamini Yesu uwapo katika shida tu? Chunguza vizuri maisha yako na mwenendo
wako wa kila siku Kiimani.
Tumsifu
Yesu Kristo!
EE
YESU TUZIDISHIE IMANI.
No hay comentarios:
Publicar un comentario