miércoles, 12 de agosto de 2015

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 19 YA MWAKA-B

JUMATANO WIKI YA 19 YA MWAKA-B
12/8/2015
Somo: Kum 34:1-12
Zab: 65
Injili: Mt 18:15-20
Nukuu:
Bwana akamwambia, Hii ndiyo nchi niliyowaapia Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo, nikisema, Nitawapa wazao wako. Basi nimekuonyesha kwa macho yako, lakini hutavuka huko,” Kum 34:4

Na ndugu yako akikukosa, enenda ukamwonye, wewe na yeye peke yenu; akikusikia, umempata nduguyo,” Mt 18:15

Na asipowasikiliza wao, liambie kanisa; na asipolisikiliza kanisa pia, na awe kwako kama mtu wa mataifa na mtoza ushuru,” Mt 18:17

Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lo lote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 18:19 

TAFAKARI: “Furaha ya Mungu tunapopatana na kuishi katika amani na upendo.”

Wapendwa wana wa Mungu, makusudi ya Mungu katika maisha yetu ni sisi sote tuishi kwa amani na upendo kama alivyotupenda yeye mwenyewe. Mungu kwa kumtuma mwanaye ulimwenguni alikuwa na makusudi hayo hayo ya kutupatanisha naye baada ya kosa la wazazi wetu wa kwanza. Pamoja na upendo huo wa Mungu Baba, bado tunaona kati yetu tunaishi kwa kutopendana na mbaya zaidi ndugu tuliozaliwa tumbo moja. Tunaishi kwa visasi na hata kutakiana mabaya.

Je, tufanyaje nini tunapokoseana kama ndugu? Yesu anatufundisha namna ya kufanya. Naye anasema hivi: Na ndugu yako akikukosa, enenda ukamwonye, wewe na yeye peke yenu; akikusikia, umempata nduguyo,” Mt 18:15. Ni vyema kama umekosana na ndugu yako mkayazungumza mkiwa naye na kupatana naye. Ni vyema mkayamaliza kama ndugu. Hamuitaji kuyakuza na kuwafaidia wengine kwa upungufu wenu. Kama hatakusikia na hayupo tayari kukusikiliza, Yesu anatupa nafasi ya pili. Naye anasema hivi: Na asipowasikiliza wao, liambie kanisa; na asipolisikiliza kanisa pia, na awe kwako kama mtu wa mataifa na mtoza ushuru,” Mt 18:17. Kanisa likiwa ndio mwili wa Yesu nasi tukiwa viungo vyake, ndiyo sehemu muhafaka wa kuyazungumza yale yote yaliyokwenda kinyuma na upendo wa Mungu. Je, tunatumia nafasi hii vyema kuyamaliza yale yanayotusibu? Kwa nini basi tunakimbilia mahakamani kwa mambo yetu ya familia? Je, tuupatapo ushindi huo wa kimahakama utatusaidia kuujenga tena ule undugu wetu ulioingia dosari? Ndugu yangu, tusipokuwa tayari kulisikiliza Kanisa tunahesabiwa kama watu wa mataifa.

Wapenda wana wa Mungu, yatupasa kuyamaliza mambo yote sisi wenyewe, na pale tunaposhindwa kufanya hivyo, basi tuliachie Kanisa litusaidie kufikia muhafaka wa matatizo yetu. Hapa ndipo penye furaha ya Mungu wetu aliye hai.Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lo lote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 18:19. Je, unataka ushindi wa kidunia au upendo wa Mungu wako aliye hai? Patana na ndugu yako kindugu, naye Mungu atakuneemesha katika haki na kweli.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU USINIPE NAFASI YA KUISHI NA KISASI. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario