JUMAPILI
YA 21 YA MWAKA-B
23/8/2015
Somo
I: Yos 24:1-2a, 15-18b
Zab:
34:1-2, 15-22
Somo
II: Efe 5:21-32
Injili:
Yoh 6:60-69
Nukuu:
“Hao watu wakajibu
wakasema, Hasha! Tusimwache Bwana, ili kuitumikia miungu mingine; kwa maana Bwana, Mungu wetu, yeye
ndiye aliyetupandisha sisi na baba zetu kutoka nchi ya Misri; kutoka nyumba ya
utumwa; naye ndiye aliyezifanya ishara zile kubwa mbele ya macho yetu, na
kutulinda katika njia ile yote tuliyoiendea, na kati ya watu wa mataifa yote
tuliopita katikati yao,” Yoh 24:16-17
“Enyi wake, watiini
waume zenu kama kumtii Bwana wetu. Kwa
maana mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni
mwokozi wa mwili,” Efe 5:22-23
“Enyi waume, wapendeni
wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake; ili makusudi alitakase na kulisafisha
kwa maji katika neno; apate
kujiletea Kanisa tukufu, lisilo na ila wala kunyanzi wala lo lote kama hayo;
bali liwe takatifu lisilo na mawaa,” Efe 5:25-27
“Lakini kama vile
Kanisa limtiivyo Kristo vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila
jambo,” Efe 5:24
“Kwa sababu hiyo mtu
atamwacha baba yake na mama yake, ataambatana na mkewe na hao wawili watakuwa
mwili mmoja,” Efe 5:31
“Roho ndiyo itiayo
uzima, mwili haufai kitu; maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima,”
Yoh 6:63
“Akasema, Kwa sababu
hiyo nimewaambia ya kwamba hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa amejaliwa
na Baba yangu,” Yoh 6:65
“Basi Simoni Petro
akamjibu, Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele. Nasi tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa
wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu,” Yoh 6:68-69
TAFAKARI:
“Tumeunganishwa na Kristo kwani Yeye anayo maneno ya uzima uzima wa milele.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 21 ya mwaka “B” wa Kanisa. Masomo yote
matatu ya leo yanatupa na kutuelezea upendo wa Mungu unaojionyesha katika
mfungamanisho wetu na Kristo. Hivyo, “tumeunganishwa na Kristo kwani yeye anayo
maneno ya uzima wa milele.” Upendo huu wa Mungu na Imani yetu juu yake bila
Kristo hakuna maana yoyote. Ukamilifu wa historia yetu ya wokovu unatimia kwa
“tendo la neno kufanyika mwili na kukaa kwetu.” Huu ni upendo mkuu ambao Mungu
kaufanya kwa watu wake.
Hivyo kwa kupitia mwono
huu wa upendo wa Mungu kwa watu wake, Waisraeli hawapo tayari kumwasi Mungu na
kuabudu miungu mingine. Nao wakasema, “tusimwache
Bwana, ili kuitumikia miungu mingine; kwa
maana Bwana, Mungu wetu, yeye ndiye aliyetupandisha sisi na baba zetu kutoka
nchi ya Misri; kutoka nyumba ya utumwa; naye ndiye aliyezifanya ishara zile
kubwa mbele ya macho yetu, na kutulinda katika njia ile yote tuliyoiendea, na
kati ya watu wa mataifa yote tuliopita katikati yao,” Yoh 24:16-17. Ndugu yangu
unaonja upendo wa Mungu katika maisha yako ya kila siku? Je, únalo lolote la
kumshukuru Mungu unapotazama historia yako kama wafanyavyo Waisraeli?
Upendo
huu wa Mungu kwa watu wake yatupasa kuuona katika mambo yote yenye kutupeleka
katika umoja wake, upendo wake, ushirikiano wake na hata katika maagano yetu
katika maisha. Ni kwa kupitia umoja huo, upendo huo, na ushirikiano huo wa
Mungu na mwanaye mpenzi, Yesu Kristo Mungu hujidhihirisha kwetu kila siku ya
maisha yetu hapa duniani. Upendo wa Mungu na mshikamano na mwanaye tunauona katika
masakramenti yake, na hasa leo tunavyotafakari kwa ukaribu sakramenti hii ya
ndoa. Naye Mtume Paulo anasema, “Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu. Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe,
kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni mwokozi wa mwili,” Efe 5:22-23.
Hapa upendo wa Mungu kupitia Kristo mwenyewe unaonekana kwa utii huu wanaoishi
wana ndoa, na hasa kwa mke kumtiii mumewe. Je, ndoa zetu leo ni salama? Akina
mama mnaishi ukweli huu katika agano lenu la ndoa? Leo baadhi ya wanawake
wamefikia kuwaita waume zao vyama chakavu. Je, hayo ndiyo makusudio ya Mungu na
muungano wenu huo?
Kwa
upande wa wanaume yawapasa kuwapenda wake zao katika kweli na haki. Upendo huu
unafananishwa na upendo wa Kristo na Kanisa lake. “Enyi waume, wapendeni
wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake; ili makusudi alitakase na kulisafisha
kwa maji katika neno; apate
kujiletea Kanisa tukufu, lisilo na ila wala kunyanzi wala lo lote kama hayo;
bali liwe takatifu lisilo na mawaa,” Efe 5:25-27. Wanaume zieshimuni ndoa zetu
kwani ndio utakatifu wenu mnapoziishi katika kweli na haki. Wake zenu
hawahitaji mambo ya pekee sana zaidi ya kuyasadifu yale wayatendayo kila siku
katika familia. Tabia ya kuwaita wake zetu magoli kipa ni chukizo mbele ya
Mungu. Muunganiko wenu ni makusudio ya Mungu, na ndivyo alivyoona inafaa.
Utii wa
kweli si utumwa kwenu, bali ni ukamilifu wa makusudio ya Mungu katika maisha ya
umilele. Wito wenu wa ndoa ni kuufikia umelele wa maisha yenu mlioandaliwa
kupitia sakramenti hiyo. Hivyo, “kama vile Kanisa
limtiivyo Kristo vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila jambo,” Efe
5:24. Ni kuwa na utii katika Kristo kwa sababu yeye anayo maneno la uzima wa
milele. Ni kwa kupitia NENO huyu vyote vilifanyika, na kwa kupitia NENO huyu
vyote huwa na uzima wa milele. “Kwa sababu hiyo mtu
atamwacha baba yake na mama yake, ataambatana na mkewe na hao wawili watakuwa
mwili mmoja,” Efe 5:31. Tendo hili la ajabu katika sakramenti hii ya ndoa
halimwesabii haki mmoja wa wanandoa kuwa na mambo yake ya pekee na binafsi
tena. Hakuna msamiati huu tena wa kusema hiki changu na hiki chako. Kwa kufanya
hivyo ni kuujeruhi mwili huu mmoja. Je, jambo hili lina ukweli katika ndoa
yako? Je, ni mambo mangapi ya siri unayoyafanya bila kumuhusisha mwenzi wako wa
ndoa? Je, hujui kwa kufanya hayo unaijeruhi ndoa yako? Ndugu yangu kama unaishi
ukweli huu na kinyume cha sakramenti hiyo ya ndoa, elewa kwamba ndoa hiyo
ishakufua katika uhalisia wa mambo na ukweli wa Kimungu. Kilicho baki ni maagizo
kuu, na wote mmekuwa wasanii katika sakramenti hii Takatifu.
Wapendwa
wana wa Mungu, hayo yote yanauzima yakiwa ndani na katika Kristo. Ni katika
roho na siyo mwili yote upata uzima. “Roho ndiyo itiayo
uzima, mwili haufai kitu; maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima,”
Yoh 6:63. Ni kwa kupitia Kristo tunapewa Roho huyu wa Mungu kuyaishi yale yote
kila mtu kadiri ya wito wake. “Kwa sababu hiyo
nimewaambia ya kwamba hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa amejaliwa na
Baba yangu,” Yoh 6:65. ‘Kristo ndiye njia, kweli, na uzima,’ Yoh 14:6.
Mafundisho
haya ya Yesu kuhusu kujiachia kwake kunakoendana na wito wa kila mmoja wetu,
yanakuwa mafundisho magumu sana kwani yanatuhitaji kujiachilia kwake kabisa.
Yatupasa kuushinda ubinadamu wetu kila siku. Yesu anapowauliza kukata tamaa kwa
wanafunzi wake na hivyo kurudi nyuma, Simoni Petro anajibu, “Bwana! Twende kwa
nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele. Nasi
tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu,” Yoh 6:68-69. Wapendwa Kristo anayo maneno ya uzima. Je, uzima
wako unaupata wapi?
Tumsifu Yesu Kristo!
No hay comentarios:
Publicar un comentario