JUMATATU WIKI YA 23 YA MWAKA-I
Somo:
Kol 1:24-2:3
Zab:
62:6-7, 9
1.
Yeye tu
ndiye mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana. Kwa Mungu
wokovu wangu, Na utukufu wangu; Mwamba wa nguvu zangu, Na kimbilio langu ni kwa
Mungu.
(K) Enyi
watu, mtumainini sikuzote, Ifunueni mioyo yenu mbele zake; Mungu ndiye kimbilio
letu.
2.
Hakika
binadamu ni ubatili, Na wenye cheo ni uongo, Katika mizani huinuka; Wote pamoja
ni hafifu kuliko ubatili. (K)
Aleluya:
Yoh 10:27
Kondoo wangu waisikia sauti
yangu;
nami
nawajua, nao wanifuata.
Injili:
Lk 6:6-11
Nukuu:
“Maana
nataka ninyi mjue jinsi ilivyo kuu juhudi yangu niliyo nayo kwa ajili yenu, na
kwa ajili ya wale wa Laodikia, na wale wasioniona uso wangu katika mwili; ili
wafarijiwe mioyo yao, wakiunganishwa katika upendo, wakapate utajiri wote wa
kufahamu kwa hakika, wapate kujua kabisa siri ya Mungu, yaani, Kristo; ambaye ndani yake yeye
hazina zote za hekima na maarifa zimesitirika,” Kol 2:1-3.
“Ndipo
Yesu akawaambia, Nawauliza ninyi, Je! Ni halali siku ya sabato kutenda mema, au
kutenda mabaya; kuponya roho au kuangamiza? Lk 6:9.
“Akawakazia
macho wote pande zote, akamwambia yule mtu, Nyosha mkono wako. Akaunyosha;
mkono wake ukawa mzima tena,” Lk 6:10.
“Wakajawa na uchungu,
wakashauriana wao kwa wao wamtendeje Yesu,” Lk 6:11.
TAFAKARI:
“…Kristo; ambaye ndani yake yeye hazina zote za hekima na maarifa
zimesitirika,” Kol 2:1-3.
Wapendwa wana wa Mungu,
ni vyema tukajiuliza swali hili kabla ya kuzama ndani zaidi katika tafakari
yetu ya leo. Kwa nini Kristo awe sababu ya kila kitu katika maisha yetu? Jibu
tunalipata kutoka Kitabu cha Matendo ya Mitume, Sura ya nne, mstari wa kumi na
mbili. Tunasoma hivi, “Wala hakuna wokovu
katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu
walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo,” Mdo 4:12. Ni katika
msingi huu wa kila kitu ndani na katika Yeye-Christocentric, Mtume
Paulo haoni haya kusema kwamba, “… sisi
tunamhubiri habari zake tukimwonya kila mtu, na kumfundisha kila mtu katika
hekima yote, tupate kumleta kila mtu mtimilifu katika Kristo,” Kol 1:24.
Mkristo bila Kristo ni ujasiri wa samaki kuishi JANGWANI. Mwisho wa ujasiri huu
ni haki ya kifo pasipo shaka.
Mtume
Paulo haona hasara ya kukosa yote na kumpata Kristo kama fahari yake, Gal 6:14.
Nguvu ya Mtume Paulo katika misioni yake yote ina msingi ndani na katika Kristo
Yesu. Kwa maantiki hiyo, Paulo anasema, “Nami najitaabisha kwa neno lilo hilo,
nikijitahidi kwa kadiri ya kutenda kazi kwake atendaye kazi ndani yangu kwa
nguvu,” Kol 1:29. Je, wewe na mimi tunao ujasiri huo kama wafuasi wake Kristo
hasa pale tunapopatwa na sintofahamu katika imani yetu? Je, twafanya juhudi
yoyote tunapolemewa na upinzani hasa kutoka kwa wampingao Kristo? Mtume Paulo
anataka wewe na mimi tuufahamu ukweli huu kama alivyowaambia
Wakolosai:-“…nataka ninyi mjue jinsi ilivyo kuu juhudi yangu niliyo nayo kwa
ajili yenu, na kwa ajili ya wale wa Laodikia, na wale wasioniona uso wangu
katika mwili; ili wafarijiwe mioyo yao, wakiunganishwa katika upendo, wakapate
utajiri wote wa kufahamu kwa hakika, wapate kujua kabisa siri ya Mungu, yaani,
Kristo; ambaye
ndani yake yeye hazina zote za hekima na maarifa zimesitirika,” Kol 2:1-3. Je,
bila Kristo waweza toboa mbingu? Ewe uliye mfuasi wa
Kristo, na mwenye kumwamini Kristo, bila Kristo u mwepesi kuliko karatasi.
Tukizama zaidi katika
Injili ya leo tunaelewa kweli hii; Kristo anatutaka tuwe na uhai, na tena tuwe
nao tele. Kristo Yesu ndiye Njia, kweli, na Uzima wetu, Yoh 14:6. Kristo akiwa
ndiye Mchungaji mwema wa kondoo zake, anajitofautisha na mwivi mwenye nia ya
kuiba na kuwachinja kondoo. Katika hili Yesu anasema, “Mwivi haji ila aibe na
kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.
Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya
kondoo,” Yoh 10:10-11. Ni kwa namna hiyo ya uchungaji mwema, na akiwa
katika sinagogi akifundisha siku ya sabato, Yesu anakutana na mtu aliyepooza
mkono, Lk 6:6. Huyu ni kondoo wake na mwenye kuhitaji uponyaji. Kwa upande wa
pili, Mafarisayo walioishikilia sheria ya sabato hasa kutokufanya kazi,
wanamtega Yesu waone atakachofanya ili wawe na sababu ya kumtia hatiani, Lk
6:7. Watu hawa hawana nia ya kuutokomeza uovu, bali kuuridhia na kuushabikia
uovu kwa manufaa yao binafsi.
Pamoja na hali na
mazingira hayo Yesu anasimamia mafundisho sahihi juu ya Upendo wa Mungu, na
kuuvunja ukimya ule wa uovu. Na ndivyo alivyo yatambua “mawazo yao, akamwambia
yule mwenye mkono uliopooza, Ondoka, simama katikati; akaondoka akasimama,” Lk
6:8. Huu ndio ujasiri wa Mkristo hai na mwenye kuiona kweli, kuisema kweli, na
kuisimamia kweli. Na baada ya kuiona kweli, kuisema kweli, na kuisimamia kweli,
“ndipo Yesu akawaambia, Nawauliza ninyi, Je! Ni halali siku ya sabato kutenda
mema, au kutenda mabaya; kuponya roho au kuangamiza?” Lk 6:9. Swali hili la
Yesu limebeba mafundisho ya kweli kuhusu huruma na upendo wa Mungu.
Lengo la Yesu hapa ni
kuziamsha kama sio kuzifufua dhamiri zao zilizokuwa zimekufa. Aulizalo Yesu kwa
Mafarisayo anakuuliza wewe na mimi pia. Na mwisho katika kuisimamia kweli
kisawa sawa, Yesu “akawakazia macho wote pande zote, akamwambia yule mtu,
Nyosha mkono wako. Akaunyosha; mkono wake ukawa mzima tena,” Lk 6:10. Na hili
ndilo anguko lao wale wauridhiao na kuushabikia uovu, “wakajawa na uchungu,
wakashauriana wao kwa wao wamtendeje Yesu,” Lk 6:11. Mwisho wa chuki ni aibu!
Leo wengi wetu kadiri ya itikadi zetu za dini, siasa, mila na desturi zetu
yawezekana tukatendeana ndivyo sivyo. Lakini elewa ndugu yangu ‘mwisho wa chuki
ni aibu’ kwani KWELI usimama mahali pake hata kama utaipindisha kwa wakati
kadiri ya nafasi na ushawishi uliokuwa nao katika jamii.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Nami najitaabisha
kwa neno lilo hilo, nikijitahidi kwa kadiri ya kutenda kazi kwake atendaye kazi
ndani yangu kwa nguvu,” Kol 1:29.
Tusali:-Ee
Yesu, tufanye vyombo vyako vya haki, kweli, Upendo na Amani. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario