jueves, 5 de septiembre de 2019

TAFAKARI: JUMAPILI YA 23 YA MWAKA-C


JUMAPILI YA 23 YA MWAKA-C
Somo I: Hek 9:13-18
Zab/Kit: 90:3-4, 5-6, 12-13, 14, 17
1.     Wamrudisha mtu mavumbini, usemapo, Rudini, enyi wanadamu. Maana miaka elfu machoni pako Ni kama siku ya jana ikiisha kupita, Na kama kesha la usiku.
(K) Wewe, Bwana, umekuwa makao yetu Kizazi baada ya kizazi
2.     Wawagharikisha, huwa kama usingizi, Asubuhi huwa kama majani yameayo. Asubuhi yachipuka na kumea, Jioni yakatika na kukauka. (K)
3.     Basi, utujulishe kuzihesabu siku zetu, Tujipatie moyo wa hekima. Ee Bwana urudi, hata lini? Uwahurumie watumishi wako. (K)
4.     Utushibishe asubuhi kwa fadhili zako, Nasi tutashangilia na kufurahi siku zetu zote. (K)
5.     Na uzuri wa Bwana, Mungu wetu, uwe juu yetu, Na kazi ya mikono yetu utufanyie thabiti, Naam, kazi ya mikono yetu uithibitishe. (K)
Somo II: Flm 9-10, 12-17
Injili: Lk 14:25-33
Nukuu
“Ni mtu yupi awezaye kulijua shauri la Mungu? Au ni nani atakayeelewa na mapenzi yake?” Hek 9:13
“Kwa kuwa mawazo ya mwanadamu yana woga, na makusudi yetu yanaelekea kushindwa,” Hek 9:14
“lakini, kwa ajili ya upendo nakusihi, kwa kuwa ni kama nilivyo, Paulo mzee, na sasa mfungwa wa Kristo Yesu pia,” Flm 9.
“Nakusihi kwa ajili ya mtoto wangu niliyemzaa katika vifungo vyangu, yaani, Onesimo; ambaye mimi nalitaka akae kwangu, apate kunitumikia badala yako katika vifungo vya Injili,” Flm 10, 13.
“Kama mtu akija kwangu naye hamchukii baba yake, na mama yake, na mke wake, na wanawe, na ndugu zake waume na wake; naam, na hata nafsi yake mwenyewe, hawezi kuwa mwanafunzi wangu,” Lk 14:26.
“Mtu ye yote asiyeuchukua msalaba wake na kuja nyuma yangu, hawezi kuwa mwanafunzi wangu,” Lk 14:27.
Basi, kadhalika kila mmoja wenu asiyeacha vyote alivyo navyo, hawezi kuwa mwanafunzi wangu,” Lk 14:33.
TAFAKARI: “Asiyeacha vyote alivyo navyo, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.”
Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 23 ya mwaka “C” wa Kanisa. Wazo kuu la leo kadiri ya masomo yetu ni juu ya upendo wa dhati ambao ni SADAKA. Upendo wa kweli ni sadaka kwa sababu unakulazimu kutoa bila kujibakiza. Kwa hali na mazingira fulani unaweza kutoa bila kupenda. Na unafanya hivyo kuondokana na karaha au usumbufu fulani, rejea habari ile ya kadhi asiye mcha Mungu, wala kujali watu, na mjane yule aliyekuwa anadai haki yake, Lk 18:1-5. Kwa upande mwingine huwezi kupenda bila kutoa. Na huwezi kama kiongozi kuwatumikia watu kama huwapendi. Na hapa ndipo tunapoona upendo wa dhati ambao ni Sadaka. Na “kabla ya sikukuu ya Pasaka, Yesu, hali akijua ya kuwa saa yake imefika, atakayotoka katika ulimwengu kwenda kwa Baba, naye ali amewapenda watu wake katika ulimwengu, aliwapenda upeo,” Yoh 13:1. Nahakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake,” Yoh 15:13. Hii ndiyo sadaka kama tunda la upendo wa dhati.
Ni wazi wewe na mimi kila mmoja anayo mapungufu yake. Hakuna aliye kamilika kwa kila kitu, na hii ndiyo hali yetu itokanayo na ubinadamu wetu. “Ni mtu yupi awezaye kulijua shauri la Mungu? Au ni nani atakayeelewa na mapenzi yake?” Hek 9:13. Kutokana na udhaifu huu twaitaji neema ya Mungu kuushinda ubinadamu wetu kuelekea ukamilifu kama Mungu alivyo mkamilifu, Mt 5:48. “Kwa kuwa mawazo ya mwanadamu yana woga, na makusudi yetu yanaelekea kushindwa,” Hek 9:14. Kwa neema ya Mungu, na sisi tukijibiidisha kuushinda ubinadamu wetu tuifikie ile mede ya dhahabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu, Flp 3:14. Tunaitaji neema ya Mungu katika hatua hii pia kwa sababu “mwili wenye uharibifu huigandamiza roho, na kiwiliwili cha kidunia huzilemea akili zilizosongwa na masumbufu,” Hek 9:15.
Pamoja na hitaji hilo la neema ya Mungu kukabiliana na yale yaliyopita nguvu na ufahamu wetu kama wanadamu, twahitaji Roho Mtakatifu kama upendo wa Mungu Baba na Mwana. Roho huyu ni alama ya Umoja na Upendo ndani yetu na wale wanaotuzunguka. Roho huyu utusaidia kuyapembua yaliyo ya Mungu na wanadamu. Ndugu yangu, “Naye ni yupi aliyeyavumbua mashauri yako, isipokuwa ulimpa Hekima na kumpelekea Roho yako takatifu kutoka juu?” Hek 9:17. Ni kwa neema za Mungu na Roho wake Mtakatifu utuwezesha kuufikia ule upendo sadaka.
Pendo Sadaka linaelezwa vizuri na kwa undani katika Injili yetu ya leo. Yesu anatupatia mapaswa ya ufuasi wetu kwake, na pendo sadaka tutakalo paswa kutoa. “Kama mtu akija kwangu naye hamchukii baba yake, na mama yake, na mke wake, na wanawe, na ndugu zake waume na wake; naam, na hata nafsi yake mwenyewe, hawezi kuwa mwanafunzi wangu,” Lk 14:26. Kumbe kuwa mwanafunzi wa Kristo ni kumpenda kwa dhati Kristo kule kuliko kwa kwanza. Tuelewe Kristo hasemi tusiwapende wazazi wetu na ndugu zetu. La hasha! bali Yeye Kristo apewa nafasi ya kwanza. Tunampa Kristo nafasi ya kwanza kwa sababu hii kubwa, naye anasema, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Wazazi wetu, ndugu, jamaa na marafiki zetu wanamwitaji Kristo kwa kuwa ndiye njia halisi, kweli kamili, na uzima wa milele ili kumfikia Baba yetu wa Mbinguni. Ni nani basi kati yetu asiyehitaji huruma na upendo wa Mungu?
Pendo hili ni sadaka kwa sababu linakutaka pia ujiachie mikononi mwa Kristo na kuachana na yale yote yanayo ipa heri na matumaini nafsi yako. “Basi, kadhalika kila mmoja wenu asiyeacha vyote alivyo navyo, hawezi kuwa mwanafunzi wangu,” Lk 14:33. Huku ndiko kujikana nafsi. Moja ya mambo makubwa ya kujikana nafsi ni kuzishika vyema na kwa ukamilifu na uaminifu amri za Mungu na neno lake. “Mkinipenda, mtazishika amri zangu. Mtu asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; nalo neno mnalolisikia silo langu, ila ni lake Baba aliyenipeleka,” Yoh 14:15, 24. Ndugu yangu unayesafiri nami kati tafakari hii, kuzishika amri na neno la Mungu kwa kupenda bila shuruti ndiko kuuchukua msalaba wa Yesu na kumfuata. “Mtu ye yote asiyeuchukua msalaba wake na kuja nyuma yangu, hawezi kuwa mwanafunzi wangu,” Lk 14:27. Na tu wanafunzi wa Yesu kama tunapendana sisi kwa sisi.
Pendo hili ni utayari wa kujitoa zaidi na zaidi kwa rafiki hadi tone la mwisho yaani, uhai uliokuwa nao kwa ajili ya wengine. “Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake,” Yoh 15:13. Wewe kama Mama au Baba katika familia unatoa pendo sadaka pale ambapo waithamini ndoa yako na familia yako na upo tayari kujitoa bila kujibakiza ili wewe upungue watoto waongezeke na Mwenzi wako wa ndoa aongezeke. Na kwa tendo hilo, Kristo ataonekana kwa watu. Nami kama Mtawa na Mkleri yanipasa kwa furaha nithamini maisha yangu ya wakfu na niwe tayari kupungua ninapotoa huduma kwa wengine bila kujibakiza ili Kristo aongezeke na kuonekana kwa watu.
Ni kwa ajili ya upendo sadaka Mtume Paulo haoni shaka kumtoa Onesimo kwa Filemoni kwa ajili ya vifungo vya Injili. “Nakusihi kwa ajili ya mtoto wangu niliyemzaa katika vifungo vyangu, yaani, Onesimo; ambaye mimi nalitaka akae kwangu, apate kunitumikia badala yako katika vifungo vya Injili,” Flm 10, 13. Naye anamwambia Filemoni, “kwa ajili ya upendo nakusihi, kwa kuwa ni kama nilivyo, Paulo mzee, na sasa mfungwa wa Kristo Yesu pia,” Flm 9. Kadiri ya mapokeo, Paulo anaandika Waraka kwa Filemoni akiwa Rumi kunako mwaka 61-63 Baada ya Kristo. Mtume Paulo anampasha habari Filemoni kwamba mtumwa wake Onesimo aliyemtoroka atarudi. “Basi kama ukiniona mimi kuwa mshirika nawe, mpokee huyu kama mimi mwenyewe,” Flm 17.
Waraka huu unafunua moyo wa Paulo na mafundisho yake juu ya utumwa, Rum 6:15. Mtume Paulo hakatazi utumwa kama ulivyokuwa zamani, bali anakazia sana kuwa bwana Mkristo lazima amjali mtumwa wake kama ndugu katika Kristo, Kol 3.22-4.1. “Lakini sikutaka kutenda neno lo lote isipokuwa kwa shauri lako, ili kwamba wema wako usiwe kama kwa lazima, bali kwa hiari,” Flm 14. Ndani na katika Kristo Yesu sisi sote ni ndugu licha ya historia zetu.
Marietha akiwa ndiye mkubwa katika familia ya watoto watano ya Mzee Jahiro, alikuwa na wakati mgumu wa kumtumza Mama yake Mzazi aliyekuwa na ugonjwa wa kupooza. Baba wa familia, yaani, Mzee Jahiro, aliuwawa kikatili kutokana na msimamo wake wa kusimamia haki kwa wote akiwa kama kiongozi wa kijiji kile.
Marietha ambaye kwa sasa ndiye muhimili wa familia, alitegemea sana biashara yake ya kuuza vocha za simu katika kituo cha mabasi. Maisha hayakuwa rahisi hata kidogo ukilinganisha kipato chake, na hitaji la familia ikiwa ni pamoja na wadogo wake wanne na mama mgonjwa. Mama Marietha muda wote alikuwa kitandani na wakati mwingine kutolewa nje endapo hali ya hewa iliruhusu. Hali hii ilimuhuzunisha sana Mama Marietha kwani alionja mzigo mzito aliokuwa nao mwanaye Marietha.
Hali hiyo ya Marietha ilimpelekea Mama yake kuyavumilia mateso na hata kukaa kimya alipohisi maumivu makali sana. Wakati mwingine ilimlazimu kutabasumu alipomwona Marietha amechoka na kukata tamaa kutokana na ugumu wa maisha. Tabasamu hili lilikuwa faraja kubwa sana kwa Marietha, na hakuacha kujitoa bila kujibakiza kwa familia yake.
Muda wote anapobaki nyumbani, Mama Marietha husali rozari hadi pale amwonapo mwanaye jioni nyumbani. Mama Marietha huikabidhi kila siku familia yake mikononi mwa Mama Bikiri Maria, na kwa namna ya pekee mwanaye Marietha ambaye ndiye mpiganaji mkubwa wa mkate wa kila siku. Baada ya miaka mitatu mambo yalibadilika sana. Marietha alifungua kituo cha huduma ya M-Pesa na duka la nguo. Waliokuwa wanasoma, yaani, wadogo zake walifaulu vizuri na kuendelea na masomo yao ya sekondari na wengine wawili chuo kikuu. Marietha alishangaa sana neema na baraka za Mungu zilivyokuwa zinammiminikia.
Siku mmoja Marietha aliwahi nyumbani mapema ili amshirikishe mama yake furaha na mafanikio yake katika biashara. Marietha alimsimulia yote mama yake na kumwambia, “ninayofuraha kubwa sana kuwa na Mama kama wewe licha ya ugonjwa ulio nao. Mama nakupenda sana kwani umenifundisha mambo mengi na hasa uvumilivu.” Huku machozi ya furaha yakimtoka, Mama Marietha alimjibu mwanaye, “Mwanangu, maisha yetu kama familia na hasa wewe kama nguzo yetu baada ya kifo cha baba yako na mimi kupooza, nilikuwa naikabidhi familia yetu kila siku mikononi mwa Mama yetu Bikira Maria, na hasa wewe. Mama huyu amekuwa kimbilio letu kila siku. Usimwache katika maisha yako.”
Siku ile ilikuwa ya furaha sana. Hata hivyo Mama Marietha aliwaomba watoto wake wasali Salamu Maria moja ili apumzike. Walifanya hivyo na kila mmoja alienda zake kulala. Kama ilivyokuwa kawaida ya Marietha kabla ya kwenda kwenye biashara zake humtakia hali mama yake, ikiwa ni pamoja na kumtengea chai. Marietha alipoingia chumbani mwa mama yake hali haikuwa kama kawaida. Mama Marietha alikuwa kesha fariki katika hali ya utulivu na tabasamu kubwa. Kutazama pembeni, Marietha aliona bahasha juu ya meza na ndani yake kulikuwa na Rozari na ujumbe huu, “kamwe usimwache Mama Bikira Maria. Ndiye anayekupigania kwa mwanaye Yesu Kristo, na kukubeba hadi leo.”
Tumsifu Yesu Kristo!
“Kwa kuwa mawazo ya mwanadamu yana woga, na makusudi yetu yanaelekea kushindwa,” Hek 9:14.
Tusali:-Ee Yesu, tujalie neema na nguvu katika kukupenda bila kujibakiza. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario