domingo, 6 de agosto de 2017

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 18 YA MWAKA-I


JUMATATU WIKI YA 18 YA MWAKA-I

Somo: Hes 11:4-15

Zab: 81:11-12, 13-14, 15-16

Injili: Mt 14:13-21

Nukuu:

“Twakumbuka samaki tuliokula huko Misri bure; na yale matango, na matikiti, na mboga, na vitunguu, na vitunguu saumu; lakini sasa roho zetu zimekauka; hapana kitu cho chote; hatuna kitu cha kutumaini isipokuwa hii mana tu,” Hes 11:5-6

“Nipate wapi nyama ya kuwapa watu hawa wote? Kwani wanililia, wakisema Tupe nyama, tupate kula,” Hes 11:13

“Mimi siwezi kuwachukua watu hawa wote peke yangu, kwa kuwa ni mzigo mzito sana wa kunishinda,” Hes 11:14

Yesu akawaambia, Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi vyakula,” Mt 14:16 

TAFAKARI: “Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi vyakula.”

Wapendwa wana wa Mungu, masomo yetu ya leo, yaani, somo la kwanza na Injili, yanaonyesha upendo na ukarimu wa Mungu wetu. Tukumbuke kuwa safari ya ukombozi wa Taifa la Israeli kutoka utumwani Misri haikuwa rahisi. Ugumu wa mioyo ya wana wa Israeli unakuwa tishio kwa Musa kuyatenda yale Mungu anayoyataka. Wana wa Israeli bado wanakumbuka maisha yao Misri licha ya utumwa waliokuwa nao huko. Hakika njaa haina adabu! “Twakumbuka samaki tuliokula huko Misri bure; na yale matango, na matikiti, na mboga, na vitunguu, na vitunguu saumu; lakini sasa roho zetu zimekauka; hapana kitu cho chote; hatuna kitu cha kutumaini isipokuwa hii mana tu,” Hes 11:5-6. Watu hawa hawaoni mkono wa Mungu katika wokovu wao. Wanadai kupewa nyama. Jambo hili linakuwa sikitiko kubwa kwa Musa, naye anasema, “Nipate wapi nyama ya kuwapa watu hawa wote? Kwani wanililia, wakisema Tupe nyama, tupate kula,” Hes 11:13. Maisha yetu ni zaidi ya kula na kunywa. Tupo hapa duniani kwa muda mfupi tu, tena tunajiandaa kwa maisha yale ya umilele. Naye Mtume Paulo anatupa angalizo juu ya kweli hii, na kusema, “…maana ufalme wa Mungu si kula wala kunywa, bali ni haki na amani na furaha katika Roho Mtakatifu,” Rum 14:17. Na huyu Roho siye yule Roho “Mtakavitu,” bali MTAKATIFU.

Musa anafikia hatua ya kukata tamaa kutokana na ugumu wa ndugu zake. “Mimi siwezi kuwachukua watu hawa wote peke yangu, kwa kuwa ni mzigo mzito sana wa kunishinda,” Hes 11:14. Ni kweli katika uongozi wetu na nafasi mbalimbali tunakutana na mizigo mizito na wakati mwingine haibebeki kiurahisi. Katika hali hii tunapata nguvu tu pale tunapomjeukia Mungu na kuwa na hofu naye.

Injili yetu ya leo tunaona ukarimu wa Mungu kwa watu wake. Yesu anawaonea huruma wale waliokuwa wanasikiliza neno lake la uzima. Kibinadamu wanafunzi wa Yesu wanatoa ushauri kwa Yesu kuwa watu waachwe waende zao vijini na kutafuta chakula. Yesu anawakumbusha wajibu wao kuwa yawapasa kuwalisha watu hao chakula. Hivyo ushauri na agizo la Yesu ni hili: “Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi vyakula,” Mt 14:16.

Wapendwa Taifa la Mungu, kwa ubatizo wetu tunashiriki ukuhani wa Kristo, unabii na ufalme wake. Hivyo kila mmoja kadiri ya wito wake anajukumu la kuwapa chakula watu wale aliwakabidhiwa. Na zaidi chakula hiki siyo tu hiki cha leo na kesho bali neno la uzima wa milele. Na juu ya neno Yesu anasema, “mbingu n anchi zitapita; lakini maneno yangu hayatapita kamwe,” Mt 24:35.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Mimi siwezi kuwachukua watu hawa wote peke yangu, kwa kuwa ni mzigo mzito sana wa kunishinda,” Hes 11:14

Tusali:-Ee Yesu nijalie neema ya kukuona wewe kwa wale wote ninaokutan nao kila siku. Amina

sábado, 5 de agosto de 2017

TAFAKARI: SIKUKUU YA KUNG'ARA KWA BWANA WETU YESU KRISTO-A


SIKUKUU YA KUNG’ARA KWA BWANA WETU YESU KRISTO

Somo I: Dan 7:9-10, 13-14

Zab: 97:1-2, 5-6, 9

Somo II: 2Pet 1:16-19

Injili: Mt 17:1-9

Nukuu:

Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa,” Dan 7:14

Maana alipata kwa Mungu Baba heshima na utukufu, hapo alipoletewa sauti iliyotoka katika utukufu mkuu, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye,” 2Pet 1:17

“akageuka sura yake mbele yao; uso wake ukang'aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama nuru,” Mt 17:2

“Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye,” Mt 17:3

“Petro akajibu akamwambia Yesu, Bwana, ni vizuri sisi kuwapo hapa; ukitaka, nitafanya hapa vibanda vitatu, kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya,” Mt 17:4

“Alipokuwa katika kusema, tazama, wingu jeupe likawatia uvuli; na tazama, sauti ikatoka katika lile wingu, ikasema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye; msikieni yeye,” Mt 17:5

“Na wale wanafunzi waliposikia, walianguka kifulifuli, wakaogopa sana,” Mt 17:6

“Yesu akaja, akawagusa, akasema, Inukeni, wala msiogope,” Mt 17:7

“Wakainua macho yao, wasione mtu ila Yesu peke yake,” Mt 17:8

“Na walipokuwa wakishuka mlimani, Yesu aliwaagiza, akasema, Msimwambie mtu ye yote habari ya maono hayo, hata Mwana wa Adamu atakapofufuka katika wafu,” Mt 17:9

TAFAKARI: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye; msikieni yeye,”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anasheherekea Sikukuu ya kung’ara kwa Bwana wetu Yesu Kristo. Tukio hili la kung’ara kwa Bwana wetu Yesu Kristo linafunua Utukufu na Umungu ya Yesu kabla na baada ya mateso na kifo chake kama sadaka iliyo hai na yenye kumpendeza Mungu. Huu ni mpango wa Mungu tangu zamani ili kumkomboa mwanadamu kutoka utumwa wa dhambi. Nabii Danieli alifunuliwa siri hii katika ndoto, na leo inatimia ndani na katika Kristo. “Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa,” Dan 7:14. Tukio hili la pekee la kung’ara kwa Bwana wetu Yesu Kristo linadhihirisha uwezo na mamlaka aliyonayo.

Wapendwa wana wa Mungu, kwa upendo usio na kipimo, wakati ulipotimia, (Ebr 1:1-2), katika historia hii ya wokovu, Mungu mwenyewe amejimwilisha na kukaa nasi. “Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli,” Yoh 1:14. Hivyo wapendwa katika Kristo, lnjili ya leo inauweka sawa ukweli huu kwa mambo makuu matatu; Dira yetu ya kufuata kama Wakristo, Utimilifu wa nyakati, na Hatma yetu iliyojengeka katika agano la umilele. Haya yote yanafanyika katika tukio hili la kung’ara kwa Bwana wetu Yesu Kristo kadiri ya simulizi la Injili ya leo.

Kwanza, ni dira yetu ya kufuata kama Wakristo. Heshima na cheo chako kama Mkristo ni utakatifu wako. Hivyo maisha yetu kama Wakristo kuelekea umilele yatafikika na kuwezekana kama ni tokeo la utakatifu wetu kwa kuyaona maisha kama ni jukumu la muda fupi hapa duniani na kama pia sehemu pekee ya maandalizi. Udhihirisho wa utakatifu huu kama dira yetu ya maisha ni tendo lile la kung’ara Kristo Yesu. “Akageuka sura yake mbele yao; uso wake ukang'aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama nuru,” Mt 17:2. Kristo anavikwa Utukufu wake ambao ataunyakua rasmi mara baada ya mateso, kifo na ufufuko huko Yerusalemu. Hivyo Utukufu wa Kristo hautenganishwi na msalaba/mateso. Kwa maana nyingine hakuna Utukufu pasipo msalaba. Kama Kristo ndiye njia, kweli na uzima, Yoh 14:6, nasi wafuasi wake itatupasa kupita njia hiyo ya msalaba, ukweli huu anaotufundisha, ili tuufikie uzima ule, yaani maisha ya milele. Kristo ni masiha ya Msalaba, nasi twamfuata Masiha wa Msalaba ili tuifikie taji ile ya Utukufu baada ya kuhesabiwa haki.

Pili, ni ukamilifu wa nyakati. Katika tendo hili la kung’ara, tunaelezwa tokeo la watu wawili, yaani Musa na Eliya katika mazungumzano na Yesu. “Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye,” Mt 17:3. Katika tendo hili, Musa anawakilisha Torati, na Eliya Unabii. Hivyo leo Yesu anaikamilisha Torati na Unabii. Naye Yesu anatuambia, “Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza. Kwa maana, amin, nawaambia, Mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka, yodi moja wala nukta moja ya torati haitaoondoka, hata yote yatimie,” Mt 5:17-18. Torati inatimilizwa kwa amri ya upendo kwa Mungu na jirani.Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii,” Mt 7:12. Ni ndani na katika Kristo tu tunapata neema na kweli kwa mkono wake. “Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo,” Yoh 1:17. Na huku ndiko kutimilika kwa sheria na kutamalaki kwa upendo, kweli, na neema.

Leo pia unabii wote ulionenwa juu ya Kristo na historia nzima ya wokovu wetu unakamilika. Unabii huu unafika ukomo wake kwa uwepo wa Kristo ambaye ni UPENDO WA MUNGU kwetu. Mtume Paulo anasema, Upendo haupungui neno wakati wo wote; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma; yakiwapo maarifa, yatabatilika,” 1Kor 13:8. Huyu ndiye Kristo Yesu! Kung’ara kwake Bwana wetu Yesu Kristo kulikoonyesha Ufukufu wake, kunaamsha furaha ya ndani ya Mtume Petro na kuyasema ya moyoni mwake. “Petro akajibu akamwambia Yesu, Bwana, ni vizuri sisi kuwapo hapa; ukitaka, nitafanya hapa vibanda vitatu, kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya,” Mt 17:4. Hata hivyo hilo halikuwa kusudi la Yesu kubaki mlimani pale. Yesu inabidi ashuke na kuukumbatia Msalaba kama alama ya ushindi na  hapo ndipo wokovu wako na wangu ulipotundikwa. Hii ndiyo safari kuelekea kilele kile cha wokovu kama Masiha wa Msalaba.

Tatu, ni hatma yetu iliyojengeka katika agano la milele. Kristo ndiye kielelezo chetu na wokovu wetu. Leo Mungu Baba anauweka ukweli huu hadharani na kusema, “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye; msikieni yeye,” Mt 17:5. Hili ndilo agano la milele kati yetu na Mungu, na Kristo akiwa ndiye daraja na mlango halisi wa sisi kupitia kwani ni kwake tu tutakuwa salama kama njia, ni kwa Kristo tu tunalishwa kweli katika kweli, na Kristo tu ndiye uzima halisi. Hivyo hapana tena ufunuo ulio wa wazi na kamili zaidi ya ufunuo huu wa Mungu kupitia mwanaye Mpenzi. Tendo hili linathibitishwa na sauti ya Mungu mwenyewe kwa viumbe vyote, Mt 17:5. Ndugu yangu, Je, unafuata sauti gani katika maisha yako? Sauti hii kutoka mbinguni inampa Yesu Kristo Heshima, Mamlaka, na Utukufu. Maana alipata kwa Mungu Baba heshima na utukufu, hapo alipoletewa sauti iliyotoka katika utukufu mkuu, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye,” 2Pet 1:17. Nasi tunapoisikia sauti hiyo na kuishi kweli hiyo, twajazwa nguvu, heshima na utukufu kwa kuishi ndani na katika Kristo.

Wapendwa wana wa Mungu, zipo sauti nyingi katika maisha yetu. Je, sauti hizo zinatupeleka karibu na Kristo Yesu au zinatutenganisha na ukweli wake? Kusikia sauti hii ni kuyafanya mapenzi yake. Na kufanya mapenzi yake maana yake ni tuyafanye kila mmoja kadiri ya wito wake.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Wakainua macho yao, wasione mtu ila Yesu peke yake,” Mt 17:8

Tusali:-Ee Yesu, tujalie neema ya kuyafanya mapenzi yako. Amina

 

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 17 YA MWAKA-I


JUMAMOSI WIKI YA 17 YA MWAKA-I

Somo: Law 25:1, 8-17

Zab: 67:1-2, 4, 6-7

Injili: Mt 14:1-12

Nukuu:

Nawe utajihesabia Sabato saba za miaka, maana, miaka saba mara saba; zitakuwa ni siku za Sabato saba za miaka kwenu, maana miaka arobaini na kenda,” Law 25:8

“Na mwaka wa hamsini mtautakasa, na kupiga mbiu ya kuachwa mahuru katika nchi yote kwa watu wote wanayokaa; itakuwa ni yubile kwenu, nanyi kila mtu atairudia milki yake mwenyewe, nanyi mtarejea kila mtu kwa jamaa yake,” Law 25:10

“Mwaka huo wa yubile mtairudia kila mtu milki yake,” Law 25:13

“Wala msidanganyane; lakini utamcha Mungu wako; kwa kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wenu,” Law 25:17

Kwa sababu Yohana alimwambia, Si halali kwako kuwa naye,” Mt 14:4

“Hata akaahidi kwa kiapo ya kwamba atampa lo lote atakaloliomba,” Mt 14:7

“Naye mfalme akasikitika; lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya wale walioketi chakulani pamoja naye, akaamuru apewe,” Mt 14:9

TAFAKARI: “Simama katika kweli na tenda haki, mche Mungu wako kwa kuwa Yeye ndiye Bwana, Mungu wako.”

Wapendwa wana wa Mungu, ni wito kwa kila mmoja wetu na hasa aliyepewa dhamana ya kuongoza kusimama katika kweli na kutenda haki. Kufanya hivyo ni kutambua na kuongozwa na hofu ya Mungu ukijua wazi kwamba ni wajibu kiimani kumcha Mungu muumba wako kwa kuwa yeye ndiye Bwana Mungu wako. Kumcha Mungu ni kufanya yale Mungu ayapendayo na yenye kuiumba taswira yake kwa viumbe vyake. Ni kutambua kwa undani kabisa kwamba uwepo wapo bila Mungu si chochote wala lolote. Ni kutambua pia hakuna uhai bila Mungu. Hofu hii ya Mungu ndiyo kieleleza cha Ibada zote hazifanyazo mwanadamu kwa kutambua uwepo wa Mungu wake kwa kila kitu akifanyacho. Tufanyapo ibada hizi isiwe ni kutimiza wajibu tu wa kiliturjia, bali tuzame katika kweli ya kile tukifanyacho kwa Imani thabiti.

Hivyo, Waisraeli katika maana hiyo hapo juu wanaifanya sabato kuwa hai kinadharia na matendo. “Nawe utajihesabia Sabato saba za miaka, maana, miaka saba mara saba; zitakuwa ni siku za Sabato saba za miaka kwenu, maana miaka arobaini na kenda,” Law 25:8. Tendo hili linapofanyika kwa miaka 49, kilele chake, yaani mwaka ule wa 50, hufanywa yote kwa matendo zaidi. Mwaka huu ujulikana kama mwaka wa jubilee. Ni wakati wa kuanza upya katika yote, kusamehe yote, kuachilia yote, na hasa wafungwa. Kwa ujumla ni mwaka wa kuishi kimatendo upendo wa Mungu. Mwaka huo wa yubile mtairudia kila mtu milki yake,” Law 25:13

Ni mwaka wa kuishi neema na baraka za Mungu. Kila mmoja alitafuta namna ya pekee kabisa kujitakasa na kuwa mpya mwili na roho. Hivyo, “mwaka wa hamsini mtautakasa, na kupiga mbiu ya kuachwa mahuru katika nchi yote kwa watu wote wanayokaa; itakuwa ni yubile kwenu, nanyi kila mtu atairudia milki yake mwenyewe, nanyi mtarejea kila mtu kwa jamaa yake,” Law 25:10. Hakika ni kipindi cha upatanisho wa kweli na kuishi katika haki na kweli ya Mungu. Hii ndiyo hofu ya Mungu itusukumayo kumcha usiku na mchana. Naye Mungu anasema, “wala msidanganyane; lakini utamcha Mungu wako; kwa kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wenu,” Law 25:17

Mpendwa, katika Injili ya leo tunaona hathari za matumizi mabaya ya madaraka yanayosababisha maafa makubwa kwa wale watetezi wa haki katika jamii inayowazunguka. Ni jambo la hatari sana kuwa na kiongozi anayeongozwa na mihehuko ya hisia zake, huku akitegemea sifa kutoka kwa watu. Kiongozi mwenye misukumo hii ya kihisia ni rahisi sana kuzikanyaga haki za wale anaowaongoza. Hii ni pamoja na kuwa makini katika ahadi azitoazo kiongozi mbele za watu. Herode anamwahidia binti yake chochote apendacho baada ya kucheza vizuri na kuufurahisha umati wa watu siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwake. Hata akaahidi kwa kiapo ya kwamba atampa lo lote atakaloliomba,” Mt 14:7. Mfalme Herode anajifunga kwa kauli yake mwenyewe. Mfalme Herode hakuwa na lakusema binti yake alipokitaka kichwa na Yohane Mbatizaji zaidi ya kutimiza ahadi yake na kulinda heshima yake kama kiongozi. Naye mfalme akasikitika; lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya wale walioketi chakulani pamoja naye, akaamuru apewe,” Mt 14:9. Je, ni watu wangapi huwa kafara kunakotokana na utafutaji wa sifa na umaarufu wa baadhi ya viongozi wetu?

Ni mbaya sana kutafuta umaarufu kwa kukanyaka haki za watu, na hasa wale ambao wapo kinyume chetu kutokana na matendo yetu yasiyo haki na hofu ya Mungu. Yohane Mbatizaji ni mhanga wa viongozi wale wenye kupenda sifa na umaarufu. Kosa la Yohane Mbatizaji ni kusimama katika kweli. Umauti unamfika Yohone Mbatizaji kwa sababu alimwambi Mfalme Herode Si halali kwako kuwa naye,” Mt 14:4. Wapo wahanga wengi wa mtindo wa Yohane Mbatizaji katika familia zetu, Jumuiya zetu ndogondogo za Kikristo, Jumuiya zetu za kitawa, Makanisani mwetu, sehemu zetu za kazi, na mbaya zaidi leo katika mfumo mzima wa utawala. Wapendwa tuutafute kwanza ufalme wa Mbinguni na mengine yote tutapewa kwa ziada.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Hata akaahidi kwa kiapo ya kwamba atampa lo lote atakaloliomba,” Mt 14:7

Tusali: Ee Yesu tujalie imani thabiti tuutafute ufalme wa mbingni. Amina

viernes, 28 de julio de 2017

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 16 YA MWAKA-I


JUMAMOSI WIKI YA 16 YA MWAKA-I

Somo: Kut 24:3-8

Zab: 50:1b-2, 5-6, 14-15

Injili: Yoh 11:19-27

Nukuu:

Musa akaenda akawaambia watu maneno yote ya Bwana, na hukumu zake zote; watu wote wakajibu kwa sauti moja, wakasema, Maneno yote aliyoyanena Bwana tutayatenda,” Kut 24:3

“Musa akaitwaa ile damu, akawanyunyizia watu, akasema, Hii ndiyo damu ya agano alilolifanya Bwana pamoja nanyi katika maneno haya yote,” Kut 24:8

“na watu wengi katika Wayahudi walikuwa wamekuja kwa Martha na Mariamu, ili kuwafariji kwa habari ya ndugu yao,” Yoh 11:19

“Basi Martha akamwambia Yesu, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa,” Yoh 11:21

“Lakini hata sasa najua ya kuwa yo yote utakayomwomba Mungu, Mungu atakupa,” Yoh 11:22

“Yesu akamwambia, Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi;” Yoh 11:25

“Akamwambia, Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimwenguni,” Yoh 11:27

TAFAKARI: “Lakini hata sasa najua ya kuwa yo yote utakayomwomba Mungu, Mungu atakupa,” Yoh 11:22.

Wapendwa wana wa Mungu, Mungu kwa nyakati mbalimbali alifanya maagano na watu wake kwa malengo mbalimbali yakilenga ushirika wake na viumbe vyake, katika safari nzima ya kuvikomboa, na hasa mwanadamu kutoka katika utumwa wa dhambi. Agano hili lilifanya kuaminiana na kutekeleza maagizo yake kwa pande zote mbili. “Musa akaenda akawaambia watu maneno yote ya Bwana, na hukumu zake zote; watu wote wakajibu kwa sauti moja, wakasema, Maneno yote aliyoyanena Bwana tutayatenda,” Kut 24:3. Mungu haikumpasa kujisainisha katika agano kwa sababu yeye mwenyewe ni UAMINIFU, na kwamwe katika Ukuu wake hawezi kwenye kinyume chake mwenyewe.

Maagano haya kama ishara ikiwa ni kielelezo kwa upande wa binadamu iliendana na uteketezaji wa viumbe vingi visivyo na doa. Damu ya viumbe hili vilihesabika kama ndiyo muhuri na kusahilisha muungano huu wa kiagano. “Musa akaitwaa ile damu, akawanyunyizia watu, akasema, Hii ndiyo damu ya agano alilolifanya Bwana pamoja nanyi katika maneno haya yote,” Kut 24:8. Hivi ni hatua za awali katika safari nzima ya mwokovu wetu. Je, kwa nini Mungu hakulifanya jambo hili mara moja tu na watu wake wakamwelewa? Bila shaka tendo na safari hii ya wokovu wa Mwanadamu umepita katika hatua mbalimbali kwa lengo la kumfanya mwanadamu huyu atambue uzuri na umaana wa thamani ya wokovu wake, na uwepo wa Mungu katika maisha yake. Ni kupitia Kristo Yesu ambaye ndiye ufunuo halisi na wawazi wa Mungu mwenyewe tumefumbuliwa kweli ya Mungu, na kwake tu, yaani neema yake,  inatosha kama asemavyo Mtume Paulo, 2Kor 12:9.

Ndugu yangu, kile alichokisema Yesu, yaani, “…mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru,” Yoh 8:32, ndicho anachotaka kukithibitisha mbele ya wanafunzi wake. Na zaidi ya hayo Yesu anakutaka wewe na mimi leo kuamini pasipo shaka yoyote kwamba Yeye ndiye njia, na kweli, na uzima; na mtu haji kwa Baba, ila kwa njia yake, Yoh 14:6. Ni katika mantiki hii Yesu anawaambia wanafunzi wake kwamba, “…Rafiki yetu, Lazaro, amelala; lakini ninakwenda nipate kumwamsha,” Yoh 11:11. Hata hivyo wanafunzi wake hawakufahamu alichomaanisha Yesu kwa maneno hayo. Tafsiri ya alichokisema Yesu ni hiki: “…alikuwa amenena habari ya mauti yake; nao walidhania ya kuwa ananena habari ya kulala usingizi. Basi hapo Yesu akawaambia waziwazi, Lazaro amekufa,” Yoh 11:13-14.

Ukweli ni kwamba hata baada ya Yesu kuiweka habari ile ya Rafiki yake wazi, yaani, Lazaro kuwa amekufa, Tomaso aitwaye Pacha-mwanafunzi wake Yesu, anabeba habari ile kwa wepesi mkubwa bila kufikiri na kuzama ndani kwa kile alichokisema Yesu. Na hivi ndivyo ilivyokuwa: “Basi Tomaso, aitwaye Pacha, akawaambia wanafunzi wenziwe, Twendeni na sisi, ili tufe pamoja naye,” Yoh 11:16. Hapa Tomaso anaonekana mtu asiye na hofu wala shaka, ila wakati utathibitisha kile alicho Tomaso. Ni Tomaso huyu huyu baada ya ufufuko wa Yesu aliyekuwa mtu mwenye mashaka mengi juu ya ufufuko wa Kristo.

Swali la kujiuliza ni hili:-ikiwa Yesu alijua fika habari ya kuumwa kwake Lazaro hadi kupatwa na mauti, kwa nini basi alijichelewesha kufika na kumponya ugonjwa wake kabla ya kufikwa na mauti hiyo? Ndugu yangu mpendwa, sehemu ya kwanza la swali hili Yesu mwenyewe kesha ijibu. Na jibu ni hili: -“Ugonjwa huu si wa mauti, bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu, ili Mwana wa Mungu atukuzwe kwa huo,” Yoh 11:4. Na sehemu ya pili ya jibu la swali hili inathibitisha kile alicho Kristo Yesu, yaani, ndani na katika Yeye ipo njia, kweli na uzima, Yoh 14:6. Na ndiyo maana kwa makusudi kabisa Yesu anafika siku ya nne baada ya kifo cha rafiki yake Lazaro. Siku ya nne ikiwa mwili waanza kuoza hakuna tena uwezekano wa kurudi katika ‘hali hai’ kadiri ya mila na desturi za kiyahudi. Hivyo “…Yesu alipofika, alimkuta amekwisha kuwamo kaburini yapata siku nne,” Yoh 11:17

Kuchelewa kwa Yesu kunaongeza uzuni na majonzi kwa dada zake Lazaro- Martha na Mariamu. “Basi Martha akamwambia Yesu, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. Lakini hata sasa najua ya kuwa yo yote utakayomwomba Mungu, Mungu atakupa,” Yoh 11:21-22, 32. Lakini ukweli ni kwamba alipo Kristo halijaharibika jambo kwa sababu, “Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:3. Yesu anawandolea hofu, mashaka, na uzuni Martha na Mariamu kwa kuthibitisha kile alicho, kwamba, “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo?” Yoh 11:25-26. Naye Martha pasipo shaka anamjibu Yesu, “Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimwenguni,” Yoh 11:27. Huzuni na majonzi haya ya Martha na Mariamu, pamoja na majirani zao, ikiwa ni pamoja na imani ile waliyokuwa nayo juu ya Kristo Yesu, inaunyong’onyeza moyo wa Yesu sana. “Yesu akalia machozi,” Yoh 11:35. Tendo hili linathibitisha pasipo shaka asili ya pili wa Yesu, yaani, ‘ubinadamu wake.’ Hakika Yesu anakupenda wewe na mimi upeo, Yoh 13:1.

Wapendwa wana wa Mungu,

“Yesu akamwambia, Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi;” Yoh 11:25

Tusali: Ee Yesu na yote yangu, usiniache hasa pale napozama katika mashaka na sintofahamu kubwa katika maisha yangu. Amina

jueves, 27 de julio de 2017

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 16 YA MWAKA-I


IJUMAA WIKI YA 16 YA MWAKA-I

Somo: Kut 20:1-17

Zab: 19:7, 8, 9, 10.

Injili: Mt 13:18-23

Nukuu:

“Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia. Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi, Bwana wako, ni Mungu mwenye wivu,” Kut 20:4-5

“Naye aliyepandwa penye udongo mzuri, huyo ndiye alisikiaye lile neno, na kuelewa nalo; yeye ndiye azaaye matunda, huyu mia, na huyu sitini, na huyu thelathini,” Mt 13:23 

TAFAKARI: “Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, bali kuwa udongo mzuri pale ulipo.”

Wapendwa wana wa Mungu, somo la kwanza la tuonyesha taswira halisi ya Mungu. Ni yeye tu tuwezaye kumsujudia na kumtumikia. Sisi binadamu tunamsujudia na kumtumikia Mungu, kwa sababu yeye ndiye alfa na omega, (Ufu 22:13) na anatuambia kuwa, “mimi Bwana, Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu; nawapatiliza wana maovu ya baba zao, hata kizazi cha tatu na cha nne cha wanichukiao,” Kut 20:5. Tunapomsaliti na kutompa mastahili yake Mungu wetu wa kweli, adhabu yake huenda hadi kizazi cha nne. Mahangaiko haya kwa upande fulani hubeba mambo yale ambayo kwayo twateseka bila kujua chanzo chake. Inawezekana jamii fulani, koo fulani, familia fulani, mahali fulani, kwa wakati fulani, walimwasi Mungu kwa matendo yao maovu na kukaa hivyo bila kufanya toba ya kweli.

Wapendwa wana wa Mungu, katika ulimwengu wa roho huwa tunarithi pia maovu na baraka. “Bwana akamwambia Abramu, Toka wewe katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonyesha; nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na kukubariki, na kulikuza jina lako; nawe uwe baraka,” Mwa 12:1-2. Huku ni kurithi baraka za Mungu.

Ukristo katika Tanzania yetu hii ya leo haujazidi ya miaka 150. Sehemu nyingi ni chini ya miaka 10 tu. Hivyo basi kati ya kizazi cha tatu na cha nne watu wengi walikuwa wanaishi nje ya ukristo kwa miaka mingi. Hivyo walitenda dhambi kama:-Kuabudu sanamu, Kuabudu miti mikubwa, Kuabudu milima, Kuabudu vyanzo vya maji, Kuabudu mizimu, Kuabudu mababu waliokufa

Hata leo wapo wanaoishi katika hali ya kufanya matambiko, mazindiko, na dhambi zinazoleta uovu kwako, ndugu zako, wanao, na wajukuu mpaka vilembwekezi. “Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia. Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi, Bwana wako, ni Mungu mwenye wivu; nawapatiliza wana maovu ya baba zao, hata kizazi cha tatu na cha nne cha wanichukiao,” Kut 20:4-5. Ndugu yangu, huku ndiko kurithi laana. Tutapata usalama tu tutakapoziacha njia hizi na kumsujudia na kumtumikia Mungu wa kweli. Naye anasema, “nami nawarehemu maelfu elfu wanipendao, na kuzishika amri zangu,” Kut 20:6.

Ndugu yangu, leo hii watu wengi wamevipa umaana vitu kuliko uhusiano wao na Mungu. Jamii yetu ya Tanzania leo tumekuwa na matukio mengi sana ya kushangaza na kusikitisha. Tunapenda utajiri wa haraka na usio wa kutoka jasho. Tunapenda madaraka pasipo kuwajibika. Tunapenda vyeo pasipo kujiandaa. Kutokana na mfumo  huu, na matamanio yake, imetufanya kama Taifa kuwa moja ya nchi katika bara letu la Afrika kuongoza kwa ushirikina. Ushirikina ni matokea ya kutokuwa na imani dhabiti. Kwa upande mwingine, ushirikia ni kuwa na imani ya nguvu fulani kutoka kwenye kitu ambacho hakina uhusiano na hicho unachokitafuta au kukifikiria.

Ni ukweli usio tia shaka kwamba, watu wengi leo hasa kwenye ulingo wa siasa, wanatumia njia zisizo rasmi kufikia malengo yao. Watu hawa wapo tayari hata kutoa maisha ya watu kama kafara kufikia malengo yao. Waathirika wakubwa katika kundi hili ni watoto wachanga na walemavu wa ngozi “maalbino.” Hofu yangu na ya walio wengi ni kuona pale vyombo vya usalama, na vyombo vya kutoa haki kama mahakama kutokufanya cho chote. Tafsiri ya wazi ni kwamba wahusika wa mambo hayo ni watu na viongozi waliopewa dhamana kubwa ya uongozi.

Kwa maana nyingine, miungu inayoabudiwa leo ni Utajiri, Uongozi, Madaraka, na Umaarufu. Ndugu yangu, “thawabu ya unyenyekevu ambao ni kumcha Bwana Ni utajiri, na heshima, nayo ni uzima.” Tuna kuwa na utajiri, heshima na uzima tunapomcha Mungu na si vinginevyo. Je, mbele ya Mungu yatupasa kujisifu kwa jambo gani? Mungu asema hivi, “ajisifuye na ajisifu kwa sababu hii, ya kwamba ananifahamu mimi, na kunijua, ya kuwa mimi ni Bwana, nitendaye wema, na hukumu, na haki, katika nchi; maana mimi napendezwa na mambo hayo, asema Bwana,” Yer 9:24.

Kwa maana nyingine, “Bwana asema hivi, Mwenye hekima asijisifu kwa sababu ya hekina yake, wala mwenye nguvu asijisifu kwa sababu ya nguvu zake, wala tajiri asijisifu kwa sababu ya utajiri wake,” Yer 9:23. Sote yatupasa kuutafuta kwanza ufalme wa Mungu. Hili ndilo kusudia la kwanza la uumbaji wetu, kwamba, “utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa,” Mt 6:23.  Tumeumbwa ili tumjue, tumpende, tumtumikie na mwisho turudi kwambe mbinguni.

Mtume Paulo anatupa sababu ya Imani yetu na ufuasi wetu kwa Kristu. Tunamuishi na kumhubiri Kristo aliyesulubiwa kwa sababu Kristo ni nguvu ya Mungu na hekima ya Mungu. Jambo hili kwa Wayahudi ni kikwazo, na Wayunani ni upuuzi. Wayahudi ni kikwazo kwa sababu kifo cha Kristo siyo mategemeo yao kwa Masiha waliyemtegemea. Masiha waliyemtegemea ni yule ambaye angewaweka huru kutoka dola ya Kirumu. Ni masiha wa kisiasa zaidi. Yesu anasema, “Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu, watumishi wangu wangenipigania, nisije nikatiwa mkononi mwa Wayahudi. Lakini ufalme wangu sio wa hapa,” Yoh 18:35. Hiki ndicho kikwazo kikubwa kwa Wayahudi. Kwa Wayunani ni upuuzi kwa mtu mwenye nguvu na mfanya miujiza kama Yesu kufa kifo cha aibu, tena cha msalaba. Kwa ufahamu na falsafa yao, jambo hili haliwezekani. Hawaoni utukufu wa msalaba zaidi ya karaha. Bali twajua, “wenye hekima wataurithi utukufu, bali kukuzwa kwa wapumbavu ni fedheha,” Mit 3:35. Yesu Kristo ndiye kielelezo na njia sahihi ya kuurithi ufalme wa Mungu.

Wapendwa wana wa Mungu, Injili ya leo inatoa ufafanuzi wa habari ile ya Mpanzi. Leo Yesu anafafanua lugha ile ya picha aliyoitumia kadiri ya mazingira na watu wake. Lengo la lugha ile ya picha kuhusu Mpanza, ni kuelezea kweli hiyo ya Mungu ndani ya mioyo yetu. Hivyo alichokifanya Mpanzi ilikuwa ni namna neno la Mungu lifanyavyo kazi ndani ya mioyo yetu na kutubadilisha. Ili neno la Mungu liwe tumaini la kweli, na ushuhuda wa kweli ndani yetu, na kwa wale wanaotuzunguka, lazima neno hilo tulisikie, tulipokee, kulitafakari, kulishirikishe, na mwisho tuwe sehemu ya neno hilo kwa kuwa mashahidi wa neno hata ikibidi kufa kwa kweli hiyo. Kulipokea neno lazima uwe na utayari wa kulisikia neno. Usipokuwa na utayari huu ni sawa na “mbegu nyingine zilianguka karibu na njia, ndege wakaja wakazila,” Mt 13:4. Na huu ndio ufafanuzi wa Yesu; “Kila mtu alisikiapo neno la ufalme asielewe nalo, huja yule mwovu, akalinyakua lililopandwa moyoni mwake. Huyo ndiye aliyepandwa karibu na njia,” Mt 13:19

Kulitafakari neno la Mungu kunakuhitaji kulisikia neno hilo na liguse maisha yako. Kutafakari neno ni kama kucheua kile ulichokula. Kama hili halikufanyika ni sawa na mbegu zile “zilizoanguka penye miamba, pasipokuwa na udongo mwingi; mara zikaota, kwa udongo kukosa kina, na jua lilipozuka ziliungua; na kwa kuwa hazina mizizi zikanyauka,” Mt 13:5-6. Na hapa Yesu anatuambia kwa kuifafanue lugha ile ya picha, kwamba, “Naye aliyepandwa penye miamba, huyo ndiye alisikiaye lile neno, akalipokea mara kwa furaha; lakini hana mizizi ndani yake, bali hudumu kwa muda; ikitukia dhiki au udhia kwa ajili ya lile neno, mara huchukizwa,” Mt 13:20-21. Kulipokea neno kwa furaha na kukosa mizizi ndani yake, ni kukosa tafakari ya kina juu ya kile ulichokisikia au kukisoma. Ni kutokulicheua neno, na hivyo neno hilo kutokuwa sehemu ya maisha yako, na kutokukupa uwezekano wa kulishirikisha kwa wengine. Huwezi kutoa usichokuwa nacho. Je, itawezekana kweli kushirikisha kwa wengine kile usichokuwa nacho?

Wapendwa wana wa Mungu, kuwa na uwezo wa kulishirikisha neno la Mungu kunategemea sana namna tunavyolicheua neno la Mungu, yaani, uwezo ule wa kulitafakari neno la Mungu na kuleta mabadiliko kwanza ndani yetu. Tunaposhindwa kufanya hivyo ni sawa na mbegu “zilizoanguka penye miiba; ile miiba ikamea, ikazisonga,” Mt 13:7. Kumbe tunaweza kushirikishana neno la Mungu vizuri pale tunapokuwa na mazingira mazuri ya kulitafakari neno la Mungu kama lilivyo, na siyo tulivyo kwa kujionea huruma. Na hapa Yesu anafafanua lughu hii ya picha na kusema, “Naye aliyepandwa penye miiba, huyo ndiye alisikiaye lile neno; na shughuli za dunia, na udanganyifu wa mali hulisonga lile neno; likawa halizai,” Mt 13:22. Leo ni wangapi tu sehemu ya Jumuiya ndogo ndogo iliyopo kwenye eneo lako, ikiwa ni pamoja na kwenda kwenye jumuiya hiyo na kuwa sehemu ya familia hiyo, ukiumega mkate na kushirikishana neno la Mungu? Leo jumuiya hizi sehemu nyingi zimekuwa kundi la watoto, akina mama, tena wajane, na wazee. Hakuna vijana, na wala hakuna akina Baba. Je, hayo malimwengu unayoyakubatia yana uzima ndani yake au umebaki kujifariji katika upumbavu? Tukifanikiwa katika hatua hii, yaani, kuliishi neno la Mungu, ni wazi tu mashahidi wazuri wa neno la Mungu ndani yetu na wale wote wanaotuzunguka.

Kuwa mashahidi na washuhuda wa neno ni sawa na mbegu zile zilizoangukapenye udongo mzuri, zikazaa, moja mia, moja sitini, moja thelathini,” Mt 13:8. Hiki ndicho atakacho Yesu kwako na kwangu, yaani, tuwe mashahidi wa kweli wa neno la Mungu. Na huu ndio ufafanuzi wa Yesu juu ya udongo mzuri: “Naye aliyepandwa penye udongo mzuri, huyo ndiye alisikiaye lile neno, na kuelewa nalo; yeye ndiye azaaye matunda, huyu mia, na huyu sitini, na huyu thelathini,” Mt 13:23. Kuzaa huku matunda kwa viwango tofauti tofauti kunatokana na nguvu ya Roho ile isukumayo ufahamu wetu juu ya neno ambalo sasa siyo tu tumelisika, bali tumelipokea. Na siyo tu tumelipokea, bali tumelitafakari kwa kina na kulicheua. Na siyo tu tumelitafakari kwa kina na kulicheua, bali kwa sasa tumelishirikisha vyema kwa wengine (uinjilishaji upya). Na mwisho siyo tu tumelishirikisha neno hilo kwa wengine bali tumekuwa sehemu ya neno hilo, kwa kuwa mashahidi na washuhuda wa kweli kwa sababu maisha yetu yanaakisi kweli hiyo. Kumbe haitoshi kufanya mambo mazuri katika ukamilifu wake, bali yakupasa kuwa mkamilifu katika maana halisi ya ukamifu kama anavyotuasa Yesu, “Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt 5:48.

Tumsifu Yesu Kristo!

Naye aliyepandwa penye udongo mzuri, huyo ndiye alisikiaye lile neno, na kuelewa nalo; yeye ndiye azaaye matunda, huyu mia, na huyu sitini, na huyu thelathini,” Mt 13:23

Tusali:-Ee Yesu Mwema, nifanye udongo mzuri ili niufunue uzuri na utukufu wako pale nilipo. Amina

 

martes, 13 de junio de 2017

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 10 YA MWAKA-1


ALHAMISI WIKI YA 10 YA MWAKA-I

Somo: 2 Kor 3:15-4:1, 3-6

Zab: 85:8ab-9, 10-11, 12-13

Injili: Mt 5:20-26

Nukuu:

“Basi ndiye Roho; walakini alipo Roho wa Bwana, hapo ndipo penye uhuru,” 2Kor 3:17

“Kwa maana hatujihubiri wenyewe, bali Kristo Yesu ya kuwa ni Bwana; na sisi wenyewe kuwa tu watumishi wenu kwa ajili ya Yesu,” 2Kor 4:5

Maana nawaambia ya kwamba, Haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni,” Mt 5:20

“Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako,” Mt 5:23

Patana na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani,” Mt 5:25

TAFAKARI: “Patana na ndugu yako uwapo pamoja naye njiani.”

Wapendwa wana wa Mungu, ni jambo la kawaida kuona ndugu wanagombana na mwisho wa siku wanaweka kando tofauti zao na kuwa kitu kimoja. Hapa sina maana ya kuchochea ugomvi nikijua kunakupatana, la hasha! Ninachosema ni kwamba ikitokea ndugu mmepishana kauli si jambo jema mkaendelea kuzibeba tofauti zenu. Ukweli ni kwamba hata kama umekosewa katika tofauti zenu, hakuna mshindi katika ugomvi huo kila mmoja akibaki na tofauti zake. Ushindi wa kweli na wa roho ni kuchukua hatua na kutafuta upatanisho hata kama wewe ndiwe uliyekosewa haki.

Ndugu yangu tunayesafiri wote katika tafakari hii, usikubali hata mara moja kumbeba yeyote katika moyo wako hasa kwa sintofahamu zilizotokana na ugomvi wenu. Kwa kukubali kuishi kwa mtindo huo ni sawa na kuuza uhuru wako na kujifungia katika chumba kidogo sana na kushindwa kutoka ilihali funguo za chumba hicho unazo mwenyewe. Usijitengenezee gereza lako mwenyewe pasipo sababu. Roho wa Mungu uliyepewa bure na kufanya makazi ndani yako unamtesa na hapo hapo unakosa neema. Toka kwenye kifungo hicho na uwe huru, na hapo Roho wa Bwana atakuwa nawe na kukupatia wingi wa neema zake. Ndugu yangu, “alipo Roho wa Bwana, hapo ndipo penye uhuru,” 2Kor 3:17.

Wapo wengi kati yetu huwa wanajisifu kwa kutoshiriki sakramenti kwa kumkomesha ndugu yake au jirani yake aliyemkosea. Utamsikia anasema kwa kujivuna, “nina mwaka mmoja na nuru si pokei Ekaristi Takatifu kwa kumkomesha kwa sababu sina muda wa kupoteza kwa kuongea naye.” Je, jambo hilo kwako ni habari njema? Ndugu yangu, huko ndiko kujihubiria mwenyewe habari za kuzimu. Kwa nini unajijengea jehenamu yako mwenyewe, tena kwa kupenda? Mtume Paulo anasema, “Kwa maana hatujihubiri wenyewe, bali Kristo Yesu ya kuwa ni Bwana; na sisi wenyewe kuwa tu watumishi wenu kwa ajili ya Yesu,” 2Kor 4:5. Yafanye maisha yako kuwa habari njema ya wokovu kila mahali uendapo na kuishi na watu. Yafanye maisha yako kuwa barua ya kusomwa na watu ili kwa kupitia kwako wamwone Kristo. “Ninyi ndinyi barua yetu, iliyoandikwa mioyoni mwetu, inajulikana na kusomwa na watu wote; mnadhihirishwa kwamba mmekuwa barua ya Kristo tuliyoikatibu, iliyoandikwa si kwa wino, bali kwa Roho wa Mungu aliye hai; si katika vibao vya mawe, ila katika vibao ambavyo ni mioyo ya nyama,” 2Kor 3:2-3.

Ndugu yangu, wapo wengi pia kati yetu ni mabingwa sana wa sura mbili mbili. Nachotaka kusema ni kwamba, wapo tunaoshiriki nao katika jumuiya ndogondogo, Kanisani, hata maisha yetu utawani ambao muda wote umebeba zigo kubwa la chuki, visasi, hasira, wivu, majivuno, na yale yote yanayofanana na haya na yasiyompendeza Mungu. Licha ya zigo hilo kuulemea Moyo, hatupo tayari kuliweka chini. Kukiwa kwenye sehemu za Ibadi huwa tunaliacha zigo hili mlangoni, na mara baada ya Ibada zigo hili tunalikimbilia na kujitwisha na mara kunaondoka nalo. Tupo tayari kulibeba zigo hili nyakati zote za majira ya mwaka, na ya Vipindi vyote vya Liturjia vya Mama Kanisa. Leo Yesu anatupa angalizo: “Maana nawaambia ya kwamba, Haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni,” Mt 5:20. Mbele za watu na jumuiya tunazoishi twajionyesha sisi ni wema na hatuna tatizo na mtu, na wakati mwingine twa tamani hata kwenda mbinguni kwa miguu yetu tukithibitisha utakatifu wetu machoni pa watu.

Wapendwa wana wa Mungu, ukitaka sala yako, na maombi yako yapate kibali mbele ya Mungu, jipatanishe wewe mwenyewe, wewe na uliyekosana naye, na pia wewe na Mungu. Hivyo “basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako,” Mt 5:23. Wengi na hasa wale tuliokosewa hupenda kuyarefusha mambo sana, na wakati mwingine tungependa tunyunyuziwe ubani kwa cheteso cha dhahabu ili tuwe tayari kwa kuyaongelea yale yaliyotutatiza.

Jambo la muhumu kupita yote kama umekosana na ndugu yako au ye yote yule, patana naye mngali injiani. Maana yake nini? Kupatana na ndugu yako mngali njiani ni kufanya juu chini kupatana na ndugu yako angali yu hai. Wengi tumeshuhudia watu hawapendi kupatana na kuishia kuapizana pasipo sababu. Wapo wengine hata baada ya kuzidiwa wakiwa kitandani karibu ya kufa wanapoomba upatanisho na ndugu yake kunakuwa na mkwamo bila mwitikio wowote na mwisho mtu huyo hufariki katika hali ya majonzi makubwa. Hivi unajisikiaje ndugu yako kufa akikuomba upatane naye nawe kwa kiburi chako hukusikia na hatimaye ndugu yako anafariki? Ndugu yangu, “Patana na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani,” Mt 5:25. Je, kwa kutokupatana na ndugu yako angali hai, utajibu nini mbele ya Kadhi-Mungu mwisho wa siku?

Tumsifu Yesu Kristo!

Maana nawaambia ya kwamba, Haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni,” Mt 5:20

Tusali:-Ee Yesu uliyempatanishi wetu na Mungu Baba, tujalie moyo wa kusemehe na kusamehewa. Amina

 

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 10 YA MWAKA-I


JUMATANO WIKI YA 10 YA MWAKA-I

Somo 2Kor 3:4-11

Zab: 99:5, 6, 7, 8, 9

Injili: Mt 5:17-19

Nukuu:

“Si kwamba twatosha sisi wenyewe kufikiri neno lo lote kwamba ni letu wenyewe, bali utoshelevu wetu watoka kwa Mungu,” 2Kor 3:5

Naye ndiye aliyetutosheleza kuwa wahudumu wa agano jipya; si wa andiko, bali wa roho; kwa maana andiko huua, bali roho huhuisha,” 2Kor 3:6

Kwa maana, ikiwa ile inayobatilika ilikuwa na utukufu, zaidi sana ile ikaayo ina utukufu,” 2Kor 3:11

Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza,” Mt 5:17

Basi mtu ye yote atakayevunja amri moja katika hizi zilizo ndogo, na kuwafundisha watu hivyo, ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni,” Mt 5:19a

“Bali mtu atakayezitenda na kuzifundisha, huyo ataitwa mkubwa katika ufalme wa mbinguni,” Mt 5:19b

TAFAKARI: “Utoshelezo wetu watoka kwa Mungu kupitia mwanaye Mpendwa Yesu Kristo.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo kwa undani tutafakari nini kitoshelezo cha mwanadamu. Ni vyema kujitazama wenyewe kwanza kabla ya kumtazama mwanadamu na utoshelezo wake kwa ujumla. Je, wajisikia kutosheka kwa hali na namna unavyoishi? Kulijibu swali hili itakupasa kuyachambua mambo haya yafuatayo; Sehemu ya kwanza jaribu kuyapitia mambo yale yote yanayokupa furaha. Ukiwa bado umebaki katika hatua hii ya kwanza kwa hayo mambo yanayokupa furaha, kila moja wapo ya hilo linalokupa furaha lilinganishe na uzima wako wa milele. Jiulize swali hili: Je, kunauhusiano wa moja kwa moja na maisha yako baada ya kifo, yaani umilele wa maisha yako? Kama hakuna uhusiano wa moja kwa moja na uzima wako wa milele, je,  mkwamo huo upo wapi? Kuchukua hatua katika mkwamo huo, yakupasa kujiona kuwa una siku ya leo tu. Hatua hiyo utakayoichukua iwe na uhusiano wa moja kwa moja na uzima wako wa milele.

Sehemu ya pili ya kutafakari utoshelezo wako jaribu kuyapitia mambo yale yote yasiyokupa furaha. Na bado ukiwa katika mambo hayo, ni vema ukajiuliza swali hili; Je, mahangaiko hayo yanautukufu mbele yake ukilinganisha na hali yako ya sasa na  umilele wa maisha yako baada ya kifo? Kama hayana, je, mkwamo wake upo wapi? Wapo wengi leo wanateseka kwa ajili ya kuteseka, na mateso yao hayana utukufu na uhusiano wa moja kwa moja na umilele wao. Mfano; kutamani nyumba nzuri ya ghorofa ya jirani yako na kutokulala usingizi ukiikodolea macho usiku kucha, hakuta kuwezesha kuwa na nyumba kama hiyo kamwe kama  hutojishughulisha na jambo lolote na hufanyi chochote kubadili hali hiyo. Ukweli ni kwamba, hakuna sababu ya kulalamika chumba kina giza wakati unashindwa kuwasha hata kijinga cha moto kuleta hata mwanga kidogo katika chumba kile.

Wapendwa katika Kristo, tunapoyatamani yale yaliyo nje ya uwezo wetu kama wanadamu twaweza kuyapata au kuyafikia kama tumefanya vyema yale yaliyochini ya uwezo wetu kama binadamu. Hapa ndipo ule msemo unapopata maana, yaani “Grace works on nature,”-“Neema hufanya kazi katika uhasili wa mazingira halisi,” na si vinginevyo. Ni kwa kulitambua jambo hili, Mtume Paulo anatoa kauli hii yenye ukomavu wa Imani: “Si kwamba twatosha sisi wenyewe kufikiri neno lo lote kwamba ni letu wenyewe, bali utoshelevu wetu watoka kwa Mungu,” 2Kor 3:5. Hii ndiyo neema ya Mungu inayotuwezesha kutoka pale tulipo na kwenda pale alipo. Utoshelevu huu kutoka kwa Mungu haudondoki tu kama mana kule jangwani, bali kwa kututaka pia tufanye yale yanayotuhusu kama wanadamu. “Aliye kuumba wewe pasipo wewe, hawezi kukukomboa wewe pasipo wewe,” Mt. Augustino wa Hippo.

Je, hali ilikuwaje kabla ya Yesu Kristo na wakati wake? Ni ukweli usiotia shaka kwamba uhusiano kati ya mwanadamu na Muumba wake ulioneka wa mbali sana, na tena wa kutisha. Mungu alionekana kama mtoa adhabu za papo kwa papo, na wakati mwingine kutafsiriwa kama mpanga mtindo fulani wa maisha ambao kwa upande wetu binadamu hata tungejitahidi kwa namna gani tusingeweza kujitoa katika hali hiyo.

Jambo la kushangaza zaidi wakati wa Yesu, Torati ile ambayo ndiyo ilikuwa mstakabali wa Taifa la wana wa Mungu-Waisraeli, ilikwisha chakachuliwa vya kutosha na hivyo Taifa hili lilikuwa linafuata Tafsiri yake tu kwa sehemu kubwa. Jambo muhimu sana la kujua ni kwamba kipindi cha Yesu Wayahudi na hasa mafarisayo na waandishi hawakuwa wanaifuata Torati kama iliyokuwa, ila tafsiri yake (maisha ya dini na matendo yake kupitia masimulizi) iliyojulikana kwa ujumla kama TALMUD. Talmud ilibeba mambo mawili: MIDRASH (tafsiri ya mambo mbalimbali toka Torati), na MISHNAH (marudio/waliyorudia au mafundisho)

Kwa mantiki hiyo hapo juu ya TALMUD, vitabu vile vitano vya Torati vingewezwa kuandikwa kwa kurasa 350 tu; wakati TALMUD ilichukuwa hadi vitabu 523; vilivyo rudufiwa (printed) katika mabando (volumes) 22. Haya ndiyo yanayonukuliwa na mafarisayo na waandishi kama mapokeo ya wazee. Sehemu nyingi za mafundisho ya Yesu anapinga jambo hili la kufuata mapokeo ambayo ni tafsiri kutoka Torati. Ni ukweli wa Mungu uliopotoshwa.

Yesu anasisitiza kuishika na kuiishi Torati kama mafundisho ya kweli ya Mungu na makusudi yake, anasema, "Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua Torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiza. Kwa maana, amini, nawaambia, Mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka, yadi moja wala nukta moja ya Torati haitaondoka, hata yote yatimie," Mt 5:17-18.

Ukweli huu wa Torati kama mafundisho na maagizo ya kweli ya Mungu waweza kuusoma pia katika sehemu nyingine za injili kama ifuatavyo;

-Mt 7:12; 12:5; 22:40;

-Lk 2:22; 10:26; 16:16; 24:44

-Yoh 1:17; 1:45; 7:19; 7:49

Yesu ni ukweli na amekuja kusimamia kweli ya Mungu akitambua ukweli huo utatuweka huru. "Basi Yesu akawaambia wale Wayahudi waliomwamini, Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo kweli itawaweka huru," Yoh 8:31-32. Ni ukweli huu anaongelea Mtume Paulo ambao utatutosheleza. “Naye ndiye aliyetutosheleza kuwa wahudumu wa agano jipya; si wa andiko, bali wa roho; kwa maana andiko huua, bali roho huhuisha,” 2Kor 3:6. Andiko hapa analolisema Mt. Paulo ni ule uchakachuaji wa Torati niliosema hapo mwanzo. Yesu Kristo amekuja kutuhuisha na ile kweli iliyokuwa tangu mwanzo, yaani Torati (mafundisho ya kweli ya Mungu na makusudio yake katika kumkomboa mwanadamu).

Ndugu yangu uliyesafiri nami katika tafakari hii, fanya tafiti moyo na uone ni mambo gani yanayokupa utoshelevu wa kweli ndani yako. La sivyo, maisha yako kama mfuasi wa Kristo yatakuwa kama mchezaji ngumu bora anayetupa makonde yake hewani mwanzo hadi mwisho wa ngumi. Je, hapa kuna ushindi? Kama tunataka ushindi, yaani, utoshelevu wa kweli ndani yetu, lazima utoke kwa Mungu, na kupitia kwa Mwanaye Mpenzi Yesu Kristo. Kwani, “amwaminiye Mwana yuna uzima wa milele; asiyemwamini Mwana hataona uzima, bali ghadhabu ya Mungu inamkalia,” Yoh 3:36

Tumsifu Yesu Kristo!

Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza,” Mt 5:17

Tusali: Ee Yesu Kristo wewe ndiye utoshelevu wetu wa kweli. Amina