JUMAMOSI WIKI YA 16 YA MWAKA-I
Somo: Kut 24:3-8
Zab: 50:1b-2, 5-6, 14-15
Injili: Yoh 11:19-27
Nukuu:
“Musa akaenda akawaambia watu maneno yote
ya Bwana, na hukumu zake zote; watu wote wakajibu kwa sauti moja, wakasema,
Maneno yote aliyoyanena Bwana tutayatenda,” Kut 24:3
“Musa akaitwaa ile
damu, akawanyunyizia watu, akasema, Hii ndiyo damu ya agano alilolifanya Bwana
pamoja nanyi katika maneno haya yote,” Kut 24:8
“na watu
wengi katika Wayahudi walikuwa wamekuja kwa Martha na Mariamu, ili kuwafariji kwa
habari ya ndugu yao,” Yoh 11:19
“Basi Martha
akamwambia Yesu, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa,” Yoh
11:21
“Lakini hata
sasa najua ya kuwa yo yote utakayomwomba Mungu, Mungu atakupa,” Yoh 11:22
“Yesu akamwambia,
Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa
anaishi;” Yoh 11:25
“Akamwambia,
Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule
ajaye ulimwenguni,” Yoh 11:27
TAFAKARI: “Lakini hata sasa
najua ya kuwa yo yote utakayomwomba Mungu, Mungu atakupa,” Yoh 11:22.
Wapendwa wana wa Mungu,
Mungu kwa nyakati mbalimbali alifanya maagano na watu wake kwa malengo
mbalimbali yakilenga ushirika wake na viumbe vyake, katika safari nzima ya
kuvikomboa, na hasa mwanadamu kutoka katika utumwa wa dhambi. Agano hili
lilifanya kuaminiana na kutekeleza maagizo yake kwa pande zote mbili. “Musa
akaenda akawaambia watu maneno yote ya Bwana, na hukumu zake zote; watu wote
wakajibu kwa sauti moja, wakasema, Maneno yote aliyoyanena Bwana tutayatenda,”
Kut 24:3. Mungu haikumpasa kujisainisha katika agano kwa sababu yeye mwenyewe
ni UAMINIFU, na kwamwe katika Ukuu wake hawezi kwenye kinyume chake mwenyewe.
Maagano haya kama
ishara ikiwa ni kielelezo kwa upande wa binadamu iliendana na uteketezaji wa
viumbe vingi visivyo na doa. Damu ya viumbe hili vilihesabika kama ndiyo muhuri
na kusahilisha muungano huu wa kiagano. “Musa akaitwaa ile damu, akawanyunyizia
watu, akasema, Hii ndiyo damu ya agano alilolifanya Bwana pamoja nanyi katika
maneno haya yote,” Kut 24:8. Hivi ni hatua za awali katika safari nzima ya
mwokovu wetu. Je, kwa nini Mungu hakulifanya jambo hili mara moja tu na watu
wake wakamwelewa? Bila shaka tendo na safari hii ya wokovu wa Mwanadamu umepita
katika hatua mbalimbali kwa lengo la kumfanya mwanadamu huyu atambue uzuri na
umaana wa thamani ya wokovu wake, na uwepo wa Mungu katika maisha yake. Ni
kupitia Kristo Yesu ambaye ndiye ufunuo halisi na wawazi wa Mungu mwenyewe
tumefumbuliwa kweli ya Mungu, na kwake tu, yaani neema yake, inatosha kama asemavyo Mtume Paulo, 2Kor
12:9.
Ndugu
yangu, kile alichokisema Yesu, yaani, “…mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli
itawaweka huru,” Yoh 8:32, ndicho anachotaka kukithibitisha mbele ya wanafunzi
wake. Na zaidi ya hayo Yesu anakutaka wewe na mimi leo kuamini pasipo shaka
yoyote kwamba Yeye ndiye njia, na kweli, na uzima; na mtu haji kwa Baba, ila
kwa njia yake, Yoh 14:6. Ni katika mantiki hii Yesu anawaambia wanafunzi wake
kwamba, “…Rafiki yetu, Lazaro, amelala; lakini ninakwenda nipate kumwamsha,” Yoh
11:11. Hata hivyo wanafunzi wake hawakufahamu alichomaanisha Yesu kwa maneno
hayo. Tafsiri ya alichokisema Yesu ni hiki: “…alikuwa amenena habari ya mauti
yake; nao walidhania ya kuwa ananena habari ya kulala usingizi. Basi hapo Yesu
akawaambia waziwazi, Lazaro amekufa,” Yoh 11:13-14.
Ukweli
ni kwamba hata baada ya Yesu kuiweka habari ile ya Rafiki yake wazi, yaani,
Lazaro kuwa amekufa, Tomaso aitwaye Pacha-mwanafunzi wake Yesu, anabeba habari
ile kwa wepesi mkubwa bila kufikiri na kuzama ndani kwa kile alichokisema Yesu.
Na hivi ndivyo ilivyokuwa: “Basi Tomaso, aitwaye Pacha, akawaambia wanafunzi
wenziwe, Twendeni na sisi, ili tufe pamoja naye,” Yoh 11:16. Hapa Tomaso
anaonekana mtu asiye na hofu wala shaka, ila wakati utathibitisha kile alicho
Tomaso. Ni Tomaso huyu huyu baada ya ufufuko wa Yesu aliyekuwa mtu mwenye
mashaka mengi juu ya ufufuko wa Kristo.
Swali
la kujiuliza ni hili:-ikiwa Yesu alijua fika habari ya kuumwa kwake Lazaro hadi
kupatwa na mauti, kwa nini basi alijichelewesha kufika na kumponya ugonjwa wake
kabla ya kufikwa na mauti hiyo? Ndugu yangu mpendwa, sehemu ya kwanza la swali
hili Yesu mwenyewe kesha ijibu. Na jibu ni hili: -“Ugonjwa huu si wa mauti,
bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu, ili Mwana wa Mungu atukuzwe kwa huo,”
Yoh 11:4. Na sehemu ya pili ya jibu la swali hili inathibitisha kile alicho
Kristo Yesu, yaani, ndani na katika Yeye ipo njia, kweli na uzima, Yoh 14:6. Na
ndiyo maana kwa makusudi kabisa Yesu anafika siku ya nne baada ya kifo cha
rafiki yake Lazaro. Siku ya nne ikiwa mwili waanza kuoza hakuna tena uwezekano
wa kurudi katika ‘hali hai’ kadiri ya mila na desturi za kiyahudi. Hivyo “…Yesu
alipofika, alimkuta amekwisha kuwamo kaburini yapata siku nne,” Yoh 11:17
Kuchelewa
kwa Yesu kunaongeza uzuni na majonzi kwa dada zake Lazaro- Martha na Mariamu.
“Basi Martha akamwambia Yesu, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu
hangalikufa. Lakini hata sasa najua ya kuwa yo yote utakayomwomba Mungu, Mungu
atakupa,” Yoh 11:21-22, 32. Lakini ukweli ni kwamba alipo Kristo halijaharibika
jambo kwa sababu, “Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika
cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:3. Yesu anawandolea hofu, mashaka, na uzuni
Martha na Mariamu kwa kuthibitisha kile alicho, kwamba, “Mimi ndimi huo ufufuo,
na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye
na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo?” Yoh 11:25-26.
Naye Martha pasipo shaka anamjibu Yesu, “Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba
wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimwenguni,” Yoh 11:27. Huzuni
na majonzi haya ya Martha na Mariamu, pamoja na majirani zao, ikiwa ni pamoja
na imani ile waliyokuwa nayo juu ya Kristo Yesu, inaunyong’onyeza moyo wa Yesu
sana. “Yesu akalia machozi,” Yoh 11:35. Tendo hili linathibitisha pasipo shaka
asili ya pili wa Yesu, yaani, ‘ubinadamu wake.’ Hakika Yesu anakupenda wewe na
mimi upeo, Yoh 13:1.
Wapendwa
wana wa Mungu,
“Yesu akamwambia,
Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa
anaishi;” Yoh 11:25
Tusali: Ee Yesu na yote
yangu, usiniache hasa pale napozama katika mashaka na sintofahamu kubwa katika
maisha yangu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario