domingo, 6 de agosto de 2017

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 18 YA MWAKA-I


JUMATATU WIKI YA 18 YA MWAKA-I

Somo: Hes 11:4-15

Zab: 81:11-12, 13-14, 15-16

Injili: Mt 14:13-21

Nukuu:

“Twakumbuka samaki tuliokula huko Misri bure; na yale matango, na matikiti, na mboga, na vitunguu, na vitunguu saumu; lakini sasa roho zetu zimekauka; hapana kitu cho chote; hatuna kitu cha kutumaini isipokuwa hii mana tu,” Hes 11:5-6

“Nipate wapi nyama ya kuwapa watu hawa wote? Kwani wanililia, wakisema Tupe nyama, tupate kula,” Hes 11:13

“Mimi siwezi kuwachukua watu hawa wote peke yangu, kwa kuwa ni mzigo mzito sana wa kunishinda,” Hes 11:14

Yesu akawaambia, Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi vyakula,” Mt 14:16 

TAFAKARI: “Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi vyakula.”

Wapendwa wana wa Mungu, masomo yetu ya leo, yaani, somo la kwanza na Injili, yanaonyesha upendo na ukarimu wa Mungu wetu. Tukumbuke kuwa safari ya ukombozi wa Taifa la Israeli kutoka utumwani Misri haikuwa rahisi. Ugumu wa mioyo ya wana wa Israeli unakuwa tishio kwa Musa kuyatenda yale Mungu anayoyataka. Wana wa Israeli bado wanakumbuka maisha yao Misri licha ya utumwa waliokuwa nao huko. Hakika njaa haina adabu! “Twakumbuka samaki tuliokula huko Misri bure; na yale matango, na matikiti, na mboga, na vitunguu, na vitunguu saumu; lakini sasa roho zetu zimekauka; hapana kitu cho chote; hatuna kitu cha kutumaini isipokuwa hii mana tu,” Hes 11:5-6. Watu hawa hawaoni mkono wa Mungu katika wokovu wao. Wanadai kupewa nyama. Jambo hili linakuwa sikitiko kubwa kwa Musa, naye anasema, “Nipate wapi nyama ya kuwapa watu hawa wote? Kwani wanililia, wakisema Tupe nyama, tupate kula,” Hes 11:13. Maisha yetu ni zaidi ya kula na kunywa. Tupo hapa duniani kwa muda mfupi tu, tena tunajiandaa kwa maisha yale ya umilele. Naye Mtume Paulo anatupa angalizo juu ya kweli hii, na kusema, “…maana ufalme wa Mungu si kula wala kunywa, bali ni haki na amani na furaha katika Roho Mtakatifu,” Rum 14:17. Na huyu Roho siye yule Roho “Mtakavitu,” bali MTAKATIFU.

Musa anafikia hatua ya kukata tamaa kutokana na ugumu wa ndugu zake. “Mimi siwezi kuwachukua watu hawa wote peke yangu, kwa kuwa ni mzigo mzito sana wa kunishinda,” Hes 11:14. Ni kweli katika uongozi wetu na nafasi mbalimbali tunakutana na mizigo mizito na wakati mwingine haibebeki kiurahisi. Katika hali hii tunapata nguvu tu pale tunapomjeukia Mungu na kuwa na hofu naye.

Injili yetu ya leo tunaona ukarimu wa Mungu kwa watu wake. Yesu anawaonea huruma wale waliokuwa wanasikiliza neno lake la uzima. Kibinadamu wanafunzi wa Yesu wanatoa ushauri kwa Yesu kuwa watu waachwe waende zao vijini na kutafuta chakula. Yesu anawakumbusha wajibu wao kuwa yawapasa kuwalisha watu hao chakula. Hivyo ushauri na agizo la Yesu ni hili: “Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi vyakula,” Mt 14:16.

Wapendwa Taifa la Mungu, kwa ubatizo wetu tunashiriki ukuhani wa Kristo, unabii na ufalme wake. Hivyo kila mmoja kadiri ya wito wake anajukumu la kuwapa chakula watu wale aliwakabidhiwa. Na zaidi chakula hiki siyo tu hiki cha leo na kesho bali neno la uzima wa milele. Na juu ya neno Yesu anasema, “mbingu n anchi zitapita; lakini maneno yangu hayatapita kamwe,” Mt 24:35.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Mimi siwezi kuwachukua watu hawa wote peke yangu, kwa kuwa ni mzigo mzito sana wa kunishinda,” Hes 11:14

Tusali:-Ee Yesu nijalie neema ya kukuona wewe kwa wale wote ninaokutan nao kila siku. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario