jueves, 5 de septiembre de 2019

TAFAKARI: JUMANNE YA WIKI YA 23 YA MWAKA-I


JUMANNE WIKI YA 23 YA MWAKA-I

Somo I: Kol 2:6-15
Zab: 145:1b-2, 8-9, 10-11
1.     Nitalihimidi jina lako milele na milele. Kila siku nitakuhimidi, Nitalisifu jina lako milele na milele.
(K) Bwana ni mwema kwa watu wote, Na rehema zake zi juu ya kazi zake zote.
2.     Bwana ana fadhili, ni mwingi wa huruma, Si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema, Bwana ni mwema kwa watu wote, Na rehema zake zi juu ya kazi zake zote. (K).
3.     Ee Bwana, kazi zako zote zitakushukuru, Na wacha Mungu wako watakuhimidi. Wataunena utukufu wa ufalme wako, Na kuuhadithia uweza wako. (K).
Aleluya: Yoh 15:16
Si ninyi mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi;
nami nikawaweka mwende mkazae matunda; na matunda yenu yapate kukaa;
ili kwamba lo lote mmwombalo Baba kwa jina langu awapeni.
Injili: Lk 6:12-19
Nukuu:
Basi kama mlivyompokea Kristo Yesu, Bwana, enendeni vivyo hivyo katika yeye,” Kol 2:6.
“wenye shina na wenye kujengwa katika yeye; mmefanywa imara kwa imani, kama mlivyofundishwa; mkizidi kutoa shukrani,” Kol 2:7.
“Hata kulipokuwa mchana aliwaita wanafunzi wake; akachagua kumi na wawili miongoni mwao, ambao aliwaita Mitume,” Lk 6:13.
“Simoni, aliyemwita jina la pili Petro, na Andrea nduguye, na Yakobo na Yohana, na Filipo na Bartolomayo, na Mathayo na Tomaso, na Yakobo wa Alfayo, na Simoni aitwaye Zelote, na Yuda wa Yakobo, na Yuda Iskariote, ndiye aliyekuwa msaliti,” Lk 6:14-16.
TAFAKARI:Basi kama mlivyompokea Kristo Yesu, Bwana, enendeni vivyo hivyo katika yeye,” Kol 2:6.
Wapendwa wana wa Mungu, imani ‘sio jambo la kujaribu na kuona tokeo lake’ kama wesemavyo wenzetu, ‘try and error.’ Wala imani sio tokeo la ‘faida katika shaka.’ Bali imani ni “…kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana,” Ebr 11:1. Kristo Yesu ni hakika ya mambo yatarajiwayo, Yoh 14:6. Ni katika mazingira haya Mtume Paulo anasisitiza jambo hili, “…kama mlivyompokea Kristo Yesu, Bwana, enendeni vivyo hivyo katika yeye,” Kol 2:6. Ukimpata Kristo katika maisha yako umepata vyote. Kwa maana nyingine, “wenye shina na wenye kujengwa katika yeye; mmefanywa imara kwa imani, kama mlivyofundishwa; mkizidi kutoa shukrani,” Kol 2:7. Na moyo usio na shukrani ukausha mema yote.
Jambo la kujiuliza ni hili, kwa nini wewe uliye batizwa na kukiri imani ndani na katika Kristo unatangatanga? Nabii Yeremia anatukumbusha jambo hili, “…Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, Amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake Na moyoni mwake amemwacha Bwana,” Yer 17:5. Ni katika mazingira haya Mtume Paulo anasema, “Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu, kwa jinsi ya mapokeo ya wanadamu, kwa jinsi ya mafundisho ya awali ya ulimwengu, wala si kwa jinsi ya Kristo,” Kol 2:8. Leo tuutazamapo ulimwengu wetu tunaona baadhi ya watu wakijiinua na kumweka Mungu katika mifuko yao na wao kuwa miungu watu.
Ndugu yangu tunayesafiri wote katika tafakari hii, ni katika Kristo tu kuna “…utimilifu wote wa Mungu, kwa jinsi ya kimwili,” Kol 2:9. Mengine yote yatokayo kwa mwanadamu ni mbwembwet tu. Wewe na mimi tumetimilika “…katika yeye aliye kichwa cha enzi yote na mamlaka,” Kol 2:10. Bila Kristo Yesu kujikweza kwako ni kupotea muda bure! Ukweli ni kwamba, ‘katika yeye tumetahiriwa kwa tohara isiyofanyika kwa mikono, kwa kuuvua mwili wa nyama, kwa tohara ya Kristo,’ Kol 2:11. Ni katika Kristo na ndani yake tumezikwa katika ubatizo, tumefufuliwa naye katika wafu, kuwa washindi kwa kufanywa hai pamoja naye akiisha kutusamehe makosa yetu, na kuwa wajasiri katika msalaba wake ambao ndio utukufu wetu kama wakristo, Kol 2:12-15. Na ndio maana twasema hakuna ‘utukufu pasipo msalaba wake Kristo.
Yesu Kristo kama kiongozi wetu na aliyeishi kile alichokisema, ili kutimiza hazma ya kile alichokijia, yaani, kumkomboa mwanadamu kutoka utumwa wa dhambi, aliyaweka yote wazi tangu mwanzo. Na kauli mbiu yake kama dira ya kila mmoja kufuata ili kufika kule alikotaka sote tufike, yaani, uzima wa milele ni hii,“Wakati umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia; tubuni, na kuiamini Injili,” Mk 1:15. Kwa maana nyingine, huruma na neema ya Mungu hufanya kazi yake pale tunapoipokea huruma na neema hiyo kwa kufanya toba ya kweli na majuto ya dhambi.
Na hata baada ya kutoa kauli mbiu yake hiyo, Yesu alionyesha wazi mpango kazi wake mwanzoni kabisa kabla ya kufanya chochote. Na mambo yalikuwa hivi; “Akaenda Nazareti, hapo alipolelewa; na siku ya sabato akaingia katika sinagogi kama ilivyokuwa desturi yake, akasimama ili asome. Akapewa chuo cha nabii Isaya, akakifungua chuo, akatafuta mahali palipoandikwa, Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa,” Lk 4:16-19. Mpango kazi mzima wa Yesu hauna uchochezi wa aina yoyote ile, wala vitisho. Ni habari njema kweli kweli na iliyojaa matumaini.
Baada ya kutoa mpango kazi wake, Yesu akiwa Mungu na Mwanadamu, alihitaji watu wa karibu naye ili kuitenda kazi ile aliyoijia kama tulivyoona hapo mwanzo. Kuwapata watu hawa, Yesu hakukurupuka, bali aliyaweka yote mikononi mwa Baba yake aliye mtuma. Hivyo, “Ikawa siku zile aliondoka akaenda mlimani ili kuomba, akakesha usiku kucha katika kumwomba Mungu,” Lk 6:12. Ni baada ya maombi haya, Yesu anawachagua wanafunzi wake. Na “hata kulipokuwa mchana aliwaita wanafunzi wake; akachagua kumi na wawili miongoni mwao, ambao aliwaita Mitume,” Lk 6:13. Hawa ndio wale Thenashara-Mitume kumi na wawili, Mt 10:2-5, yaani, “Simoni, aliyemwita jina la pili Petro, na Andrea nduguye, na Yakobo na Yohana, na Filipo na Bartolomayo, na Mathayo na Tomaso, na Yakobo wa Alfayo, na Simoni aitwaye Zelote, na Yuda wa Yakobo, na Yuda Iskariote, ndiye aliyekuwa msaliti,” Lk 6:14-16.
Hawa Thenashara ndio waliokuwa wasaidizi wake wa karibu katika kutimiza lile alilolijia yaani, kukuweka wewe na mimi huru kutoka utumwa wa dhambi. Na hawa Thenashara, “akawapa uwezo na mamlaka juu ya pepo wote na kuponya maradhi,” Lk 9:1. ‘Aliwapa mamlaka’ ikimaanisha uhuru wa kufanya yale yampendezayo Mungu. Katika kweli hii, Yesu aliruhusu ubunifu katika utendaji kila mmoja kadiri ya karama zake. Hakika Kristo Yesu ni Kiongozi kweli kweli, na mfano kwetu ulio hai. Tujifunze kwake.
Baada ya kufanikisha mpango huu, ikiwa ni pamoja na kuweka wazi kauli mbiu yake, Mk 1:15, mpango kazi wake, Lk 4:16-19, na kuwachagua watu wake wa karibu, yaani, Thenashara, Lk 6:14-16, alianza mara moja kazi ile aliyoijia. Hivyo “waliokuja kumsikiliza na kuponywa magonjwa yao; na wale waliosumbuliwa na pepo wachafu; waliponywa. Na makutano yote walikuwa wakitaka kumgusa, kwa sababu uweza ulikuwa ukimtoka ukiwaponya wote,” Lk 6:17b-19. Yesu kamwe hakupoteza muda wake kupambana na watesi wake. Kwa maana nyingine, Yesu hakuwa na muda wa kupoteza kupambana na wapinzani wake; Mafarisayo, Waandishi, na Wazee, bali aliutumia muda wake wote wa miaka ile mitatu kuhubiri Habari Njema za Ufalme wa Mbinguni. Matokeo ya kazi yake ni uwepo wa wewe na mimi leo kama Wakristo na wafuasi wake wenye hofu ya Mungu. Ni wajibu msingi kwa matiki hiyo kwamba wewe na mimi yatupasa kuwa mawakili wa Kristo pale tulipo.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Na ninyi mlipokuwa mmekufa kwa sababu ya makosa yenu na kutokutahiriwa kwa mwili wenu, aliwafanya hai pamoja naye, akiisha kutusamehe makosa yote,” Kol 2:13.
Tusali:-Ee Yesu mwema, nifanye wakili wako wema pale nilipo kila kadiri ya wito na karama ulizonijalia. Amina

TAFAKARI: JUMATATU YA WIKI YA 23 YA MWAKA-I


JUMATATU WIKI YA 23 YA MWAKA-I

Somo: Kol 1:24-2:3
Zab: 62:6-7, 9
1.     Yeye tu ndiye mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana. Kwa Mungu wokovu wangu, Na utukufu wangu; Mwamba wa nguvu zangu, Na kimbilio langu ni kwa Mungu.
(K) Enyi watu, mtumainini sikuzote, Ifunueni mioyo yenu mbele zake; Mungu ndiye kimbilio letu.
2.     Hakika binadamu ni ubatili, Na wenye cheo ni uongo, Katika mizani huinuka; Wote pamoja ni hafifu kuliko ubatili. (K)
Aleluya: Yoh 10:27
Kondoo wangu waisikia sauti yangu;
nami nawajua, nao wanifuata.
Injili: Lk 6:6-11
Nukuu:
“Maana nataka ninyi mjue jinsi ilivyo kuu juhudi yangu niliyo nayo kwa ajili yenu, na kwa ajili ya wale wa Laodikia, na wale wasioniona uso wangu katika mwili; ili wafarijiwe mioyo yao, wakiunganishwa katika upendo, wakapate utajiri wote wa kufahamu kwa hakika, wapate kujua kabisa siri ya Mungu, yaani, Kristo; ambaye ndani yake yeye hazina zote za hekima na maarifa zimesitirika,” Kol 2:1-3.
“Ndipo Yesu akawaambia, Nawauliza ninyi, Je! Ni halali siku ya sabato kutenda mema, au kutenda mabaya; kuponya roho au kuangamiza? Lk 6:9.
“Akawakazia macho wote pande zote, akamwambia yule mtu, Nyosha mkono wako. Akaunyosha; mkono wake ukawa mzima tena,” Lk 6:10.
“Wakajawa na uchungu, wakashauriana wao kwa wao wamtendeje Yesu,” Lk 6:11.
TAFAKARI: “…Kristo; ambaye ndani yake yeye hazina zote za hekima na maarifa zimesitirika,” Kol 2:1-3.
Wapendwa wana wa Mungu, ni vyema tukajiuliza swali hili kabla ya kuzama ndani zaidi katika tafakari yetu ya leo. Kwa nini Kristo awe sababu ya kila kitu katika maisha yetu? Jibu tunalipata kutoka Kitabu cha Matendo ya Mitume, Sura ya nne, mstari wa kumi na mbili. Tunasoma hivi, “Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo,” Mdo 4:12. Ni katika msingi huu wa kila kitu ndani na katika Yeye-Christocentric, Mtume Paulo haoni haya kusema kwamba, … sisi tunamhubiri habari zake tukimwonya kila mtu, na kumfundisha kila mtu katika hekima yote, tupate kumleta kila mtu mtimilifu katika Kristo,” Kol 1:24. Mkristo bila Kristo ni ujasiri wa samaki kuishi JANGWANI. Mwisho wa ujasiri huu ni haki ya kifo pasipo shaka.
Mtume Paulo haona hasara ya kukosa yote na kumpata Kristo kama fahari yake, Gal 6:14. Nguvu ya Mtume Paulo katika misioni yake yote ina msingi ndani na katika Kristo Yesu. Kwa maantiki hiyo, Paulo anasema, “Nami najitaabisha kwa neno lilo hilo, nikijitahidi kwa kadiri ya kutenda kazi kwake atendaye kazi ndani yangu kwa nguvu,” Kol 1:29. Je, wewe na mimi tunao ujasiri huo kama wafuasi wake Kristo hasa pale tunapopatwa na sintofahamu katika imani yetu? Je, twafanya juhudi yoyote tunapolemewa na upinzani hasa kutoka kwa wampingao Kristo? Mtume Paulo anataka wewe na mimi tuufahamu ukweli huu kama alivyowaambia Wakolosai:-“…nataka ninyi mjue jinsi ilivyo kuu juhudi yangu niliyo nayo kwa ajili yenu, na kwa ajili ya wale wa Laodikia, na wale wasioniona uso wangu katika mwili; ili wafarijiwe mioyo yao, wakiunganishwa katika upendo, wakapate utajiri wote wa kufahamu kwa hakika, wapate kujua kabisa siri ya Mungu, yaani, Kristo; ambaye ndani yake yeye hazina zote za hekima na maarifa zimesitirika,” Kol 2:1-3. Je, bila Kristo waweza toboa mbingu? Ewe uliye mfuasi wa Kristo, na mwenye kumwamini Kristo, bila Kristo u mwepesi kuliko karatasi.
Tukizama zaidi katika Injili ya leo tunaelewa kweli hii; Kristo anatutaka tuwe na uhai, na tena tuwe nao tele. Kristo Yesu ndiye Njia, kweli, na Uzima wetu, Yoh 14:6. Kristo akiwa ndiye Mchungaji mwema wa kondoo zake, anajitofautisha na mwivi mwenye nia ya kuiba na kuwachinja kondoo. Katika hili Yesu anasema, “Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele. Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo,” Yoh 10:10-11. Ni kwa namna hiyo ya uchungaji mwema, na akiwa katika sinagogi akifundisha siku ya sabato, Yesu anakutana na mtu aliyepooza mkono, Lk 6:6. Huyu ni kondoo wake na mwenye kuhitaji uponyaji. Kwa upande wa pili, Mafarisayo walioishikilia sheria ya sabato hasa kutokufanya kazi, wanamtega Yesu waone atakachofanya ili wawe na sababu ya kumtia hatiani, Lk 6:7. Watu hawa hawana nia ya kuutokomeza uovu, bali kuuridhia na kuushabikia uovu kwa manufaa yao binafsi.
Pamoja na hali na mazingira hayo Yesu anasimamia mafundisho sahihi juu ya Upendo wa Mungu, na kuuvunja ukimya ule wa uovu. Na ndivyo alivyo yatambua “mawazo yao, akamwambia yule mwenye mkono uliopooza, Ondoka, simama katikati; akaondoka akasimama,” Lk 6:8. Huu ndio ujasiri wa Mkristo hai na mwenye kuiona kweli, kuisema kweli, na kuisimamia kweli. Na baada ya kuiona kweli, kuisema kweli, na kuisimamia kweli, “ndipo Yesu akawaambia, Nawauliza ninyi, Je! Ni halali siku ya sabato kutenda mema, au kutenda mabaya; kuponya roho au kuangamiza?” Lk 6:9. Swali hili la Yesu limebeba mafundisho ya kweli kuhusu huruma na upendo wa Mungu.
Lengo la Yesu hapa ni kuziamsha kama sio kuzifufua dhamiri zao zilizokuwa zimekufa. Aulizalo Yesu kwa Mafarisayo anakuuliza wewe na mimi pia. Na mwisho katika kuisimamia kweli kisawa sawa, Yesu “akawakazia macho wote pande zote, akamwambia yule mtu, Nyosha mkono wako. Akaunyosha; mkono wake ukawa mzima tena,” Lk 6:10. Na hili ndilo anguko lao wale wauridhiao na kuushabikia uovu, “wakajawa na uchungu, wakashauriana wao kwa wao wamtendeje Yesu,” Lk 6:11. Mwisho wa chuki ni aibu! Leo wengi wetu kadiri ya itikadi zetu za dini, siasa, mila na desturi zetu yawezekana tukatendeana ndivyo sivyo. Lakini elewa ndugu yangu ‘mwisho wa chuki ni aibu’ kwani KWELI usimama mahali pake hata kama utaipindisha kwa wakati kadiri ya nafasi na ushawishi uliokuwa nao katika jamii.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Nami najitaabisha kwa neno lilo hilo, nikijitahidi kwa kadiri ya kutenda kazi kwake atendaye kazi ndani yangu kwa nguvu,” Kol 1:29.
Tusali:-Ee Yesu, tufanye vyombo vyako vya haki, kweli, Upendo na Amani. Amina

TAFAKARI: JUMAPILI YA 23 YA MWAKA-C


JUMAPILI YA 23 YA MWAKA-C
Somo I: Hek 9:13-18
Zab/Kit: 90:3-4, 5-6, 12-13, 14, 17
1.     Wamrudisha mtu mavumbini, usemapo, Rudini, enyi wanadamu. Maana miaka elfu machoni pako Ni kama siku ya jana ikiisha kupita, Na kama kesha la usiku.
(K) Wewe, Bwana, umekuwa makao yetu Kizazi baada ya kizazi
2.     Wawagharikisha, huwa kama usingizi, Asubuhi huwa kama majani yameayo. Asubuhi yachipuka na kumea, Jioni yakatika na kukauka. (K)
3.     Basi, utujulishe kuzihesabu siku zetu, Tujipatie moyo wa hekima. Ee Bwana urudi, hata lini? Uwahurumie watumishi wako. (K)
4.     Utushibishe asubuhi kwa fadhili zako, Nasi tutashangilia na kufurahi siku zetu zote. (K)
5.     Na uzuri wa Bwana, Mungu wetu, uwe juu yetu, Na kazi ya mikono yetu utufanyie thabiti, Naam, kazi ya mikono yetu uithibitishe. (K)
Somo II: Flm 9-10, 12-17
Injili: Lk 14:25-33
Nukuu
“Ni mtu yupi awezaye kulijua shauri la Mungu? Au ni nani atakayeelewa na mapenzi yake?” Hek 9:13
“Kwa kuwa mawazo ya mwanadamu yana woga, na makusudi yetu yanaelekea kushindwa,” Hek 9:14
“lakini, kwa ajili ya upendo nakusihi, kwa kuwa ni kama nilivyo, Paulo mzee, na sasa mfungwa wa Kristo Yesu pia,” Flm 9.
“Nakusihi kwa ajili ya mtoto wangu niliyemzaa katika vifungo vyangu, yaani, Onesimo; ambaye mimi nalitaka akae kwangu, apate kunitumikia badala yako katika vifungo vya Injili,” Flm 10, 13.
“Kama mtu akija kwangu naye hamchukii baba yake, na mama yake, na mke wake, na wanawe, na ndugu zake waume na wake; naam, na hata nafsi yake mwenyewe, hawezi kuwa mwanafunzi wangu,” Lk 14:26.
“Mtu ye yote asiyeuchukua msalaba wake na kuja nyuma yangu, hawezi kuwa mwanafunzi wangu,” Lk 14:27.
Basi, kadhalika kila mmoja wenu asiyeacha vyote alivyo navyo, hawezi kuwa mwanafunzi wangu,” Lk 14:33.
TAFAKARI: “Asiyeacha vyote alivyo navyo, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.”
Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 23 ya mwaka “C” wa Kanisa. Wazo kuu la leo kadiri ya masomo yetu ni juu ya upendo wa dhati ambao ni SADAKA. Upendo wa kweli ni sadaka kwa sababu unakulazimu kutoa bila kujibakiza. Kwa hali na mazingira fulani unaweza kutoa bila kupenda. Na unafanya hivyo kuondokana na karaha au usumbufu fulani, rejea habari ile ya kadhi asiye mcha Mungu, wala kujali watu, na mjane yule aliyekuwa anadai haki yake, Lk 18:1-5. Kwa upande mwingine huwezi kupenda bila kutoa. Na huwezi kama kiongozi kuwatumikia watu kama huwapendi. Na hapa ndipo tunapoona upendo wa dhati ambao ni Sadaka. Na “kabla ya sikukuu ya Pasaka, Yesu, hali akijua ya kuwa saa yake imefika, atakayotoka katika ulimwengu kwenda kwa Baba, naye ali amewapenda watu wake katika ulimwengu, aliwapenda upeo,” Yoh 13:1. Nahakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake,” Yoh 15:13. Hii ndiyo sadaka kama tunda la upendo wa dhati.
Ni wazi wewe na mimi kila mmoja anayo mapungufu yake. Hakuna aliye kamilika kwa kila kitu, na hii ndiyo hali yetu itokanayo na ubinadamu wetu. “Ni mtu yupi awezaye kulijua shauri la Mungu? Au ni nani atakayeelewa na mapenzi yake?” Hek 9:13. Kutokana na udhaifu huu twaitaji neema ya Mungu kuushinda ubinadamu wetu kuelekea ukamilifu kama Mungu alivyo mkamilifu, Mt 5:48. “Kwa kuwa mawazo ya mwanadamu yana woga, na makusudi yetu yanaelekea kushindwa,” Hek 9:14. Kwa neema ya Mungu, na sisi tukijibiidisha kuushinda ubinadamu wetu tuifikie ile mede ya dhahabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu, Flp 3:14. Tunaitaji neema ya Mungu katika hatua hii pia kwa sababu “mwili wenye uharibifu huigandamiza roho, na kiwiliwili cha kidunia huzilemea akili zilizosongwa na masumbufu,” Hek 9:15.
Pamoja na hitaji hilo la neema ya Mungu kukabiliana na yale yaliyopita nguvu na ufahamu wetu kama wanadamu, twahitaji Roho Mtakatifu kama upendo wa Mungu Baba na Mwana. Roho huyu ni alama ya Umoja na Upendo ndani yetu na wale wanaotuzunguka. Roho huyu utusaidia kuyapembua yaliyo ya Mungu na wanadamu. Ndugu yangu, “Naye ni yupi aliyeyavumbua mashauri yako, isipokuwa ulimpa Hekima na kumpelekea Roho yako takatifu kutoka juu?” Hek 9:17. Ni kwa neema za Mungu na Roho wake Mtakatifu utuwezesha kuufikia ule upendo sadaka.
Pendo Sadaka linaelezwa vizuri na kwa undani katika Injili yetu ya leo. Yesu anatupatia mapaswa ya ufuasi wetu kwake, na pendo sadaka tutakalo paswa kutoa. “Kama mtu akija kwangu naye hamchukii baba yake, na mama yake, na mke wake, na wanawe, na ndugu zake waume na wake; naam, na hata nafsi yake mwenyewe, hawezi kuwa mwanafunzi wangu,” Lk 14:26. Kumbe kuwa mwanafunzi wa Kristo ni kumpenda kwa dhati Kristo kule kuliko kwa kwanza. Tuelewe Kristo hasemi tusiwapende wazazi wetu na ndugu zetu. La hasha! bali Yeye Kristo apewa nafasi ya kwanza. Tunampa Kristo nafasi ya kwanza kwa sababu hii kubwa, naye anasema, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Wazazi wetu, ndugu, jamaa na marafiki zetu wanamwitaji Kristo kwa kuwa ndiye njia halisi, kweli kamili, na uzima wa milele ili kumfikia Baba yetu wa Mbinguni. Ni nani basi kati yetu asiyehitaji huruma na upendo wa Mungu?
Pendo hili ni sadaka kwa sababu linakutaka pia ujiachie mikononi mwa Kristo na kuachana na yale yote yanayo ipa heri na matumaini nafsi yako. “Basi, kadhalika kila mmoja wenu asiyeacha vyote alivyo navyo, hawezi kuwa mwanafunzi wangu,” Lk 14:33. Huku ndiko kujikana nafsi. Moja ya mambo makubwa ya kujikana nafsi ni kuzishika vyema na kwa ukamilifu na uaminifu amri za Mungu na neno lake. “Mkinipenda, mtazishika amri zangu. Mtu asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; nalo neno mnalolisikia silo langu, ila ni lake Baba aliyenipeleka,” Yoh 14:15, 24. Ndugu yangu unayesafiri nami kati tafakari hii, kuzishika amri na neno la Mungu kwa kupenda bila shuruti ndiko kuuchukua msalaba wa Yesu na kumfuata. “Mtu ye yote asiyeuchukua msalaba wake na kuja nyuma yangu, hawezi kuwa mwanafunzi wangu,” Lk 14:27. Na tu wanafunzi wa Yesu kama tunapendana sisi kwa sisi.
Pendo hili ni utayari wa kujitoa zaidi na zaidi kwa rafiki hadi tone la mwisho yaani, uhai uliokuwa nao kwa ajili ya wengine. “Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake,” Yoh 15:13. Wewe kama Mama au Baba katika familia unatoa pendo sadaka pale ambapo waithamini ndoa yako na familia yako na upo tayari kujitoa bila kujibakiza ili wewe upungue watoto waongezeke na Mwenzi wako wa ndoa aongezeke. Na kwa tendo hilo, Kristo ataonekana kwa watu. Nami kama Mtawa na Mkleri yanipasa kwa furaha nithamini maisha yangu ya wakfu na niwe tayari kupungua ninapotoa huduma kwa wengine bila kujibakiza ili Kristo aongezeke na kuonekana kwa watu.
Ni kwa ajili ya upendo sadaka Mtume Paulo haoni shaka kumtoa Onesimo kwa Filemoni kwa ajili ya vifungo vya Injili. “Nakusihi kwa ajili ya mtoto wangu niliyemzaa katika vifungo vyangu, yaani, Onesimo; ambaye mimi nalitaka akae kwangu, apate kunitumikia badala yako katika vifungo vya Injili,” Flm 10, 13. Naye anamwambia Filemoni, “kwa ajili ya upendo nakusihi, kwa kuwa ni kama nilivyo, Paulo mzee, na sasa mfungwa wa Kristo Yesu pia,” Flm 9. Kadiri ya mapokeo, Paulo anaandika Waraka kwa Filemoni akiwa Rumi kunako mwaka 61-63 Baada ya Kristo. Mtume Paulo anampasha habari Filemoni kwamba mtumwa wake Onesimo aliyemtoroka atarudi. “Basi kama ukiniona mimi kuwa mshirika nawe, mpokee huyu kama mimi mwenyewe,” Flm 17.
Waraka huu unafunua moyo wa Paulo na mafundisho yake juu ya utumwa, Rum 6:15. Mtume Paulo hakatazi utumwa kama ulivyokuwa zamani, bali anakazia sana kuwa bwana Mkristo lazima amjali mtumwa wake kama ndugu katika Kristo, Kol 3.22-4.1. “Lakini sikutaka kutenda neno lo lote isipokuwa kwa shauri lako, ili kwamba wema wako usiwe kama kwa lazima, bali kwa hiari,” Flm 14. Ndani na katika Kristo Yesu sisi sote ni ndugu licha ya historia zetu.
Marietha akiwa ndiye mkubwa katika familia ya watoto watano ya Mzee Jahiro, alikuwa na wakati mgumu wa kumtumza Mama yake Mzazi aliyekuwa na ugonjwa wa kupooza. Baba wa familia, yaani, Mzee Jahiro, aliuwawa kikatili kutokana na msimamo wake wa kusimamia haki kwa wote akiwa kama kiongozi wa kijiji kile.
Marietha ambaye kwa sasa ndiye muhimili wa familia, alitegemea sana biashara yake ya kuuza vocha za simu katika kituo cha mabasi. Maisha hayakuwa rahisi hata kidogo ukilinganisha kipato chake, na hitaji la familia ikiwa ni pamoja na wadogo wake wanne na mama mgonjwa. Mama Marietha muda wote alikuwa kitandani na wakati mwingine kutolewa nje endapo hali ya hewa iliruhusu. Hali hii ilimuhuzunisha sana Mama Marietha kwani alionja mzigo mzito aliokuwa nao mwanaye Marietha.
Hali hiyo ya Marietha ilimpelekea Mama yake kuyavumilia mateso na hata kukaa kimya alipohisi maumivu makali sana. Wakati mwingine ilimlazimu kutabasumu alipomwona Marietha amechoka na kukata tamaa kutokana na ugumu wa maisha. Tabasamu hili lilikuwa faraja kubwa sana kwa Marietha, na hakuacha kujitoa bila kujibakiza kwa familia yake.
Muda wote anapobaki nyumbani, Mama Marietha husali rozari hadi pale amwonapo mwanaye jioni nyumbani. Mama Marietha huikabidhi kila siku familia yake mikononi mwa Mama Bikiri Maria, na kwa namna ya pekee mwanaye Marietha ambaye ndiye mpiganaji mkubwa wa mkate wa kila siku. Baada ya miaka mitatu mambo yalibadilika sana. Marietha alifungua kituo cha huduma ya M-Pesa na duka la nguo. Waliokuwa wanasoma, yaani, wadogo zake walifaulu vizuri na kuendelea na masomo yao ya sekondari na wengine wawili chuo kikuu. Marietha alishangaa sana neema na baraka za Mungu zilivyokuwa zinammiminikia.
Siku mmoja Marietha aliwahi nyumbani mapema ili amshirikishe mama yake furaha na mafanikio yake katika biashara. Marietha alimsimulia yote mama yake na kumwambia, “ninayofuraha kubwa sana kuwa na Mama kama wewe licha ya ugonjwa ulio nao. Mama nakupenda sana kwani umenifundisha mambo mengi na hasa uvumilivu.” Huku machozi ya furaha yakimtoka, Mama Marietha alimjibu mwanaye, “Mwanangu, maisha yetu kama familia na hasa wewe kama nguzo yetu baada ya kifo cha baba yako na mimi kupooza, nilikuwa naikabidhi familia yetu kila siku mikononi mwa Mama yetu Bikira Maria, na hasa wewe. Mama huyu amekuwa kimbilio letu kila siku. Usimwache katika maisha yako.”
Siku ile ilikuwa ya furaha sana. Hata hivyo Mama Marietha aliwaomba watoto wake wasali Salamu Maria moja ili apumzike. Walifanya hivyo na kila mmoja alienda zake kulala. Kama ilivyokuwa kawaida ya Marietha kabla ya kwenda kwenye biashara zake humtakia hali mama yake, ikiwa ni pamoja na kumtengea chai. Marietha alipoingia chumbani mwa mama yake hali haikuwa kama kawaida. Mama Marietha alikuwa kesha fariki katika hali ya utulivu na tabasamu kubwa. Kutazama pembeni, Marietha aliona bahasha juu ya meza na ndani yake kulikuwa na Rozari na ujumbe huu, “kamwe usimwache Mama Bikira Maria. Ndiye anayekupigania kwa mwanaye Yesu Kristo, na kukubeba hadi leo.”
Tumsifu Yesu Kristo!
“Kwa kuwa mawazo ya mwanadamu yana woga, na makusudi yetu yanaelekea kushindwa,” Hek 9:14.
Tusali:-Ee Yesu, tujalie neema na nguvu katika kukupenda bila kujibakiza. Amina

TAFAKARI: JUMAMOSI YA WIKI YA 22 YA MWAKA-I


JUMAMOSI WIKI YA 22 YA MWAKA-I
Somo: Kol 1:21-23
Zab: 54:2-3, 5 na 7.
1      Ee Mungu, uyasikie maombi yangu, Uyasikilize maneno ya kinywa changu. Kwa maana wageni wamenishambulia; Watu watishao wananitafuta nafsi yangu; Hawakumweka Mungu mbele yao.
(K) Bwana ndiye msaada wangu
2      Atawarudishia adui zangu ubaya wao; Uwaangamize kwa uaminifu wako. Kwa kuwa limeniokoa na kila taabu; Na jicho langu limeridhika Kwa kuwatazama adui zangu. (K)
Injili: Lk 6:1-5
Nukuu:
Na ninyi, mliokuwa hapo kwanza mmefarikishwa, tena adui katika nia zenu, kwa matendo yenu mabaya, amewapatanisha sasa; katika mwili wa nyama yake, kwa kufa kwake,” Kol 1:21-22a.
“Akawaambia, Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato,” Lk 6:5.
TAFAKARI: “Kristo katuweka huru, hivyo tusimame katika kweli kila siku.”
Wapendwa wana Mungu, Kristo katuweka huru, hivyo tusimame katika kweli kila siku. Kusimama katika kweli ni kuthamini na kuishi kweli ya Mungu na kuwa na hofu yake. Hofu ya Mungu tuliyonayo msingi wake ni upendo wa Mungu hasa kwa kumtoa mwanaye mpenzi kama sadaka, na kututoa kutoka utumwa wa dhambi. Ukombozi wetu ni wa gharama kubwa sana. Je, wauthamini Ukristo wako kwa kuishi Imani ya kweli? Mtume Paulo anatukumbusha habari hii kwa kusema, “Na ninyi, mliokuwa hapo kwanza mmefarikishwa, tena adui katika nia zenu, kwa matendo yenu mabaya, amewapatanisha sasa; katika mwili wa nyama yake, kwa kufa kwake,” Kol 1:21-22a.
Ni kwa mantiki hiyo hapo juu kwamba Kristo ndiye kielelezo cha yote yale tuyafanyayo ili tuurithi ufalme wa Mbingini tulioandaliwa na kuutamani. Je, yale yote niyafanyayo leo na sasa yanaendana na sadaka ya Yesu pale msalabani? Yesu anataka Wayahudi, na wewe na mimi tuelewe kwamba yale tuyafanyayo yaendane na thamani ya upendo wa Mungu kwetu, na Yeye, yaani Kristo ndiye msingi wa vyote. Kristo akiwa msingi wa maisha yetu na sababu ya yale yote tuyafanyayo, basi tutakuwa huru kweli kweli kwa sababu tutajua ni nini tunayemtumikia. Hivyo Yesu anawaambia Wayahudi “Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato,” Lk 6:5. Kristo ndiye mizania ya kweli kuhusu Mungu tunayemwamini na kumwabudu. Kristo ndiye anayejua siri ya ufalme wa Mungu, na kwa kupitia Yeye nasi tunafunuliwa siri hiyo. Ndugu yangu Kristo ndiye njia, kweli na uzima, Yoh 14:6.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Akawaambia, Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato,” Lk 6:5.
Tusali:-Ee Yesu kwako tu huru.

TAFAKARI: IJUMAA YA WIKI YA 22 YA MWAKA-I


IJUMAA WIKI YA 22 YA MWAKA-I
Somo: Kol 1:15-20
Zab: 100: 1b-2, 3, 4,5
1      Dunia yote; Mtumikieni Bwana kwa furaha; Njoni mbele zake kwa kuimba.
(K) Njoni mbele zake Bwana kwa kuimba.
2      Jueni kwamba Bwana ndiye Mungu; Ndiye aliyetuumba na sisi tu watu wake; Tu watu wake, na kondoo wa malisho yake. (K)
3      Ingieni malangoni mwake kwa kushukuru; Nyuani mwake kwa kusifu; Mshukuruni, lihimidini jina lake. (K)
4      Kwa kuwa Bwana ndiye mwema; Rehema zake ni za milele; Na uaminifu wake vizazi na vizazi. (K)
Injili: Lk 5:33-39
Kwa kuwa katika yeye vitu vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi, vinavyoonekana na visivyoonekana; ikiwa ni vitu vya enzi, au usultani, au enzi, au mamlaka; vitu vyote viliumbwa kwa njia yake, na kwa ajili yake,” Kol 1:16.
Lakini Yesu akawaambia, Je! Mwaweza kuwafanya wafunge walioalikwa arusini, akiwapo bwana arusi pamoja nao?” Lk 5:34.
“Lakini divai mpya sharti kutiwa katika viriba vipya,” Lk 5:38.
“Wala hakuna anywaye divai ya kale akatamani divai mpya; kwa kuwa asema, Ile ya kale ndiyo iliyo njema,” Lk 5:39.
TAFAKARI: “Nguvu na mamlaka ya Kristo ni uthibitisho wa ujemedari wake dhidi ya uovu.”
Wapendwa wana wa Mungu, mamlaka aliyokuwa nayo Yesu ni vita na ushindi dhidi ya uovu hapa duniani. Ni ukweli usiopingika kwa kupitia jina lake tunapata uponyaji wa kweli, Mdo 4:12. “Lakini Petro akasema, Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilicho nacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama uende,” Mdo 3:6. “Mamlaka ya Yesu yamejengwa chini ya mamlaka ya Mungu. Hivyo hakuna jambo lolote alifanyalo Yesu Lisilo kuwa na uhusiano na Mungu, huku jambo lile likifunua siri ya Mungu kila kukichwa. “Kwa kuwa katika yeye vitu vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi, vinavyoonekana na visivyoonekana; ikiwa ni vitu vya enzi, au usultani, au enzi, au mamlaka; vitu vyote viliumbwa kwa njia yake, na kwa ajili yake,” Kol 1:16. Kwa nini basi nakuwa na mashaka juu ya utendaji wa Kristo katika maisha yangu?
Wapendwa katika Kristo, Yesu anapotoa mfano wa vazi kuukuu na jipya, na kwa upande mwingine divai ya zamani na kiriba cha kipya anataka kutufundisha jambo hili; kwanza kabisa lazima tujue sababu na malengo ya maisha yetu hapa tuniani. Hatupo hapa duniani kwa bahati mbaya hata kidogo. Tupo katika ulimwengu huu kadiri ya mpango wa Mungu ambao ni dhahiri na mathubuti. Hivyo lolote lile lililo jema mbele ya Mungu huwiishwa na kufanya upya. Katika Injili ya leo tunaona watu wakimletea Yesu malalamiko juu ya kufunga na kuomba. Kufunga kwetu na kuomba kwetu uifaidia kwanza kabisa roho zetu na wenzetu. Tunawajibu huo kiimani, na yatupasa kuutekeleza pasipo imani na msaada wowote. Ndiyo maana Yesu anawauliza watesi wake swali hili: “Je! Mwaweza kuwafanya wafunge walioalikwa arusini, akiwapo bwana arusi pamoja nao?” Lk 5:34. Maisha yapaswa kusherehekewa kwa sababu ni mali na zawadi ya Mungu.
Hivyo basi, upya wetu kiimani hutoshelezwa na upya tuupokeao kwa Yesu tunaposhiriki sakramenti zake tukiwa katika hali ya usafi. Hivyo “divai mpya sharti kutiwa katika viriba vipya,” Lk 5:38. Ndani na katika Kristo kiimani hujengeka kwa matendo madogo madogo yanayompendeza Mungu. “Wala hakuna anywaye divai ya kale akatamani divai mpya; kwa kuwa asema, Ile ya kale ndiyo iliyo njema,” Lk 5:39. Ndugu yangu ukiona vinaelea ujue vimeundwa.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Lakini divai mpya sharti kutiwa katika viriba vipya,” Lk 5:38.
Tusali:-Ee Yesu Mwema, tuimarishe katika imani, na tuishi katika kweli yako. Amina

miércoles, 4 de septiembre de 2019

TAFAKARI: ALHAMISI YA WIKI YA 22 YA MWAKA-I


ALHAMISI WIKI YA 22 YA MWAKA-I
Somo: Kol 1:9-14
Zab: 98: 2-3ab, 3cd-4, 5-6
1      Bwana ameufunua wokovu wake, Machoni pa mataifa ameidhihirisha haki yake. Amezikumbuka rehema zake, Na uaminifu wake kwa nyumba ya Israeli.
(K) Bwana ameufunua wokovu wake, Machoni pa mataifa ameidhihirisha haki yake.
2      Miisho yote ya dunia imeuona Wokovu wa Mungu wetu. Mshangilieni Bwana, nchi yote, Inueni sauti, imbeni kwa furaha, imbeni zaburi. (K)
3      Mwimbieni Bwana zaburi kwa kinubi, Kwa kinubi na sauti ya zaburi. Kwa panda na sauti ya baragumu. Shangilieni mbele za Mfalme, Bwana.
Injili: Lk 5:1-11
Nukuu:
“mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana, mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu,” Kol 1:10.
“Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake; ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi,” Kol 1:13-14.
Hata alipokwisha kunena, alimwambia Simoni, Tweka mpaka kilindini, mkashushe nyavu zenu mvue samaki,” Lk 5:4.
“Simoni akajibu akamwambia, Bwana mkubwa, tumefanya kazi ya kuchosha usiku kucha, tusipate kitu; lakini kwa neno lako nitazishusha nyavu,” Lk 5:5.
“Simoni Petro alipoona hayo, alianguka magotini pa Yesu, akisema, Ondoka kwangu, kwa kuwa mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana,” Lk 5:8.
“Yesu akamwambia Simoni, Usiogope, tangu sasa utakuwa ukivua watu,” Lk 5:10b.
TAFAKARI: “Kama ushakutana na Kristo katika Maisha yako lazima akubadili mwenendo wako.”
Wapendwa wana wa Mungu, yawezekana hadi leo licha ya kuingizwa katika urika wa wana wa Mungu na warithi wa ufalme wake kwa sakramenti ya ubatizo, bado haujawahi kukutana na Kristo katika maana ya kuguswa kuliko ndani kabisa ya maisha yako. Tunakutana na Kristo pale tu tunapoanza kuyachukulia maisha yetu na ufuasi wetu kwake kwa namna iliyo hai na ya kuguswa kwa yale yote tuyafanyayo ndani na katika Kristo Yesu. Mara tuifikiapo hatua na hali hii, tendo hili haliwi tena tendo au swala la kihisia, hadithi au simulizi fulani la kufikirika, bali maisha halisi.
Ndugu yangu, maisha halisi ndani na katika Kristo yanatuwajibisha kwa kila namna, tunapendezwa nayo, maisha hayo huzaa matunda mema, na mwisho maisha hayo utuongezea ufahamu juu ya Mungu. Ni kwa mantiki hii Mtume Paulo anawasihi Wakolosai nasi pia kwamba, “tuenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana, mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu,” Kol 1:10. Tunawajibika kuuona ukweli huu tunapopima uzito wa dhambi na wokovu aliotupatia Kristo kwa sadaka ya Kifo chake pale msalabani. Hakika ni upendo mkubwa sana kwetu wanadamu. Kristo ndiye pekee anayetuweka huru kutoka nguvu za giza na kutuingiza katika ufalme wa Mungu kwa pendo lake, kwa sababu ni kwake tu kwenye ukombozi na msamaha wa dhambi zetu. Hivyo Kristo, “alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake; ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi,” Kol 1:13-14. Je, ndugu yangu una sababu yoyote ya kuacha kumsamehe mwenzako kwa vigezo vyovyote vile  ulivyo navyo? Ukristo na ufuasi wangu kwake una maana gani ninapotazama tendo hili la msamaha? Nisipobadilika katika tendo hili hakika bado sijakutana na Kristo Yesu.
Ndugu zangu, mahangaiko katika maisha yetu ya kila siku yasiwe ukuta wa kutokuona uwepo na nguvu ya Kristo Yesu ndani ya yale tuyafanyayo hata kama tunauzoefu nayo. Kama kweli wasadiki Kristo ndiye Mwokozi, basi ni kwa namna hiyo hiyo huyaweza yote yaliyo chini ya miguu yake kwa sababu, “amevitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya kanisa; ambalo ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote,” Efe 1:22-23. Yesu Kristo analiweka jambo hili hadharani anapowakuta Simon Petro na wenzake waliokuwa mahodari wa kuvua samaki usiku kucha bila kupata chochote. Naye Yesu anamwambia Simoni, “Tweka mpaka kilindini, mkashushe nyavu zenu mvue samaki,” Lk 5:4. Kwa maana nyingine Yesu anamwambia Simoni Petro kwamba “jaribu tena pasipo kuwa na shaka na urushe kete yako ya mwisho katika ukamilifu wote.” Maneno haya ya Yesu yanamtia shaka kidogo Simoni Petro kutokana na uzoefu aliokuwa nao katika kuvua samaki. Hata hivyo Simoni anamwamini Yesu pasipo shaka na kufanya alivyoagizwa. Hivyo, “Simoni akajibu akamwambia, Bwana mkubwa, tumefanya kazi ya kuchosha usiku kucha, tusipate kitu; lakini kwa neno lako nitazishusha nyavu,” Lk 5:5. Ndugu zangu, “ni kwa neno lake Yesu, Simoni Petro anazishusha nyavu.” Ni kwa njia ya neno Mungu aliumba ulimwengu kutoka utupu. Hivyo ni kwa neno hili: “Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika. Ndani yake ndimo ulimokuwa uzima, nao ule uzima ulikuwa nuru ya watu,” Yoh 1:3-4. Je, bado unamashaka na Neno wa Mungu, yaani Yesu Kristo?
Muujiza wa wingi wa samaki uliotokana na hali isiyoyakawaida kadiri ya ufahamu aliokuwa nao Simoni juu ya uvuvi unamfanya akutane na Kristo katika maisha halisi na kujiona alivyo kiroho. Hapa ndipo pale tunaposema kwamba unapokutana na Kristo ndani na katika Yeye lazima akubadilishe. Kubadilishwa kwa Simoni kunajionyesha katika hali ya dhambi iliyoisuta nafsi yake. Hivyo katika mguso huu, “Simoni Petro alipoona hayo, alianguka magotini pa Yesu, akisema, Ondoka kwangu, kwa kuwa mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana,” Lk 5:8. Je, ninapokutana na matendo makuu ya Mungu katika maisha yangu nauona udhaifu wangu? Je, matendo hayo makuu ya Mungu ni mastahili yangu yanayotokana na mafanikio yangu na juhudi zangu bila mkono wa Mungu?
Wapendwa wana wa Mungu, tunapokutana na Kristo katika uhalisia wa maisha yetu ya kila siku, hali hiyo hughubikwa na hofu kubwa kwa sababu tunajiona kama tulivyo kwani Kristo huwa kioo cha kujitazamia nafsi na roho yetu. Tupatapo hali hiyo, tusisahau kuwa Yesu anatuambia kama alivyo mwambia Simoni, “Usiogope, tangu sasa utakuwa ukivua watu,” Lk 5:10b. Maana yake yake, “usihofu kwani ninakuandaa kwa makubwa zaidi ya hayo niliyokutendea.” Mungu wetu mara zote utuwazia mambo makubwa zaidi ya yale tuyafanyayo kila siku, na neema na baraka anazotujalia pasipo mastahili yetu, Yer 29:11.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Simoni akajibu akamwambia, Bwana mkubwa, tumefanya kazi ya kuchosha usiku kucha, tusipate kitu; lakini kwa neno lako nitazishusha nyavu,” Lk 5:5.
Tusali:-Ee Yesu, matendo yako kwangu ni ya ajabu sana! Utukuzwe na kuheshimiwa milele. Amina