domingo, 6 de agosto de 2017

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 18 YA MWAKA-I


JUMATATU WIKI YA 18 YA MWAKA-I

Somo: Hes 11:4-15

Zab: 81:11-12, 13-14, 15-16

Injili: Mt 14:13-21

Nukuu:

“Twakumbuka samaki tuliokula huko Misri bure; na yale matango, na matikiti, na mboga, na vitunguu, na vitunguu saumu; lakini sasa roho zetu zimekauka; hapana kitu cho chote; hatuna kitu cha kutumaini isipokuwa hii mana tu,” Hes 11:5-6

“Nipate wapi nyama ya kuwapa watu hawa wote? Kwani wanililia, wakisema Tupe nyama, tupate kula,” Hes 11:13

“Mimi siwezi kuwachukua watu hawa wote peke yangu, kwa kuwa ni mzigo mzito sana wa kunishinda,” Hes 11:14

Yesu akawaambia, Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi vyakula,” Mt 14:16 

TAFAKARI: “Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi vyakula.”

Wapendwa wana wa Mungu, masomo yetu ya leo, yaani, somo la kwanza na Injili, yanaonyesha upendo na ukarimu wa Mungu wetu. Tukumbuke kuwa safari ya ukombozi wa Taifa la Israeli kutoka utumwani Misri haikuwa rahisi. Ugumu wa mioyo ya wana wa Israeli unakuwa tishio kwa Musa kuyatenda yale Mungu anayoyataka. Wana wa Israeli bado wanakumbuka maisha yao Misri licha ya utumwa waliokuwa nao huko. Hakika njaa haina adabu! “Twakumbuka samaki tuliokula huko Misri bure; na yale matango, na matikiti, na mboga, na vitunguu, na vitunguu saumu; lakini sasa roho zetu zimekauka; hapana kitu cho chote; hatuna kitu cha kutumaini isipokuwa hii mana tu,” Hes 11:5-6. Watu hawa hawaoni mkono wa Mungu katika wokovu wao. Wanadai kupewa nyama. Jambo hili linakuwa sikitiko kubwa kwa Musa, naye anasema, “Nipate wapi nyama ya kuwapa watu hawa wote? Kwani wanililia, wakisema Tupe nyama, tupate kula,” Hes 11:13. Maisha yetu ni zaidi ya kula na kunywa. Tupo hapa duniani kwa muda mfupi tu, tena tunajiandaa kwa maisha yale ya umilele. Naye Mtume Paulo anatupa angalizo juu ya kweli hii, na kusema, “…maana ufalme wa Mungu si kula wala kunywa, bali ni haki na amani na furaha katika Roho Mtakatifu,” Rum 14:17. Na huyu Roho siye yule Roho “Mtakavitu,” bali MTAKATIFU.

Musa anafikia hatua ya kukata tamaa kutokana na ugumu wa ndugu zake. “Mimi siwezi kuwachukua watu hawa wote peke yangu, kwa kuwa ni mzigo mzito sana wa kunishinda,” Hes 11:14. Ni kweli katika uongozi wetu na nafasi mbalimbali tunakutana na mizigo mizito na wakati mwingine haibebeki kiurahisi. Katika hali hii tunapata nguvu tu pale tunapomjeukia Mungu na kuwa na hofu naye.

Injili yetu ya leo tunaona ukarimu wa Mungu kwa watu wake. Yesu anawaonea huruma wale waliokuwa wanasikiliza neno lake la uzima. Kibinadamu wanafunzi wa Yesu wanatoa ushauri kwa Yesu kuwa watu waachwe waende zao vijini na kutafuta chakula. Yesu anawakumbusha wajibu wao kuwa yawapasa kuwalisha watu hao chakula. Hivyo ushauri na agizo la Yesu ni hili: “Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi vyakula,” Mt 14:16.

Wapendwa Taifa la Mungu, kwa ubatizo wetu tunashiriki ukuhani wa Kristo, unabii na ufalme wake. Hivyo kila mmoja kadiri ya wito wake anajukumu la kuwapa chakula watu wale aliwakabidhiwa. Na zaidi chakula hiki siyo tu hiki cha leo na kesho bali neno la uzima wa milele. Na juu ya neno Yesu anasema, “mbingu n anchi zitapita; lakini maneno yangu hayatapita kamwe,” Mt 24:35.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Mimi siwezi kuwachukua watu hawa wote peke yangu, kwa kuwa ni mzigo mzito sana wa kunishinda,” Hes 11:14

Tusali:-Ee Yesu nijalie neema ya kukuona wewe kwa wale wote ninaokutan nao kila siku. Amina

sábado, 5 de agosto de 2017

TAFAKARI: SIKUKUU YA KUNG'ARA KWA BWANA WETU YESU KRISTO-A


SIKUKUU YA KUNG’ARA KWA BWANA WETU YESU KRISTO

Somo I: Dan 7:9-10, 13-14

Zab: 97:1-2, 5-6, 9

Somo II: 2Pet 1:16-19

Injili: Mt 17:1-9

Nukuu:

Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa,” Dan 7:14

Maana alipata kwa Mungu Baba heshima na utukufu, hapo alipoletewa sauti iliyotoka katika utukufu mkuu, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye,” 2Pet 1:17

“akageuka sura yake mbele yao; uso wake ukang'aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama nuru,” Mt 17:2

“Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye,” Mt 17:3

“Petro akajibu akamwambia Yesu, Bwana, ni vizuri sisi kuwapo hapa; ukitaka, nitafanya hapa vibanda vitatu, kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya,” Mt 17:4

“Alipokuwa katika kusema, tazama, wingu jeupe likawatia uvuli; na tazama, sauti ikatoka katika lile wingu, ikasema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye; msikieni yeye,” Mt 17:5

“Na wale wanafunzi waliposikia, walianguka kifulifuli, wakaogopa sana,” Mt 17:6

“Yesu akaja, akawagusa, akasema, Inukeni, wala msiogope,” Mt 17:7

“Wakainua macho yao, wasione mtu ila Yesu peke yake,” Mt 17:8

“Na walipokuwa wakishuka mlimani, Yesu aliwaagiza, akasema, Msimwambie mtu ye yote habari ya maono hayo, hata Mwana wa Adamu atakapofufuka katika wafu,” Mt 17:9

TAFAKARI: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye; msikieni yeye,”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anasheherekea Sikukuu ya kung’ara kwa Bwana wetu Yesu Kristo. Tukio hili la kung’ara kwa Bwana wetu Yesu Kristo linafunua Utukufu na Umungu ya Yesu kabla na baada ya mateso na kifo chake kama sadaka iliyo hai na yenye kumpendeza Mungu. Huu ni mpango wa Mungu tangu zamani ili kumkomboa mwanadamu kutoka utumwa wa dhambi. Nabii Danieli alifunuliwa siri hii katika ndoto, na leo inatimia ndani na katika Kristo. “Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa,” Dan 7:14. Tukio hili la pekee la kung’ara kwa Bwana wetu Yesu Kristo linadhihirisha uwezo na mamlaka aliyonayo.

Wapendwa wana wa Mungu, kwa upendo usio na kipimo, wakati ulipotimia, (Ebr 1:1-2), katika historia hii ya wokovu, Mungu mwenyewe amejimwilisha na kukaa nasi. “Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli,” Yoh 1:14. Hivyo wapendwa katika Kristo, lnjili ya leo inauweka sawa ukweli huu kwa mambo makuu matatu; Dira yetu ya kufuata kama Wakristo, Utimilifu wa nyakati, na Hatma yetu iliyojengeka katika agano la umilele. Haya yote yanafanyika katika tukio hili la kung’ara kwa Bwana wetu Yesu Kristo kadiri ya simulizi la Injili ya leo.

Kwanza, ni dira yetu ya kufuata kama Wakristo. Heshima na cheo chako kama Mkristo ni utakatifu wako. Hivyo maisha yetu kama Wakristo kuelekea umilele yatafikika na kuwezekana kama ni tokeo la utakatifu wetu kwa kuyaona maisha kama ni jukumu la muda fupi hapa duniani na kama pia sehemu pekee ya maandalizi. Udhihirisho wa utakatifu huu kama dira yetu ya maisha ni tendo lile la kung’ara Kristo Yesu. “Akageuka sura yake mbele yao; uso wake ukang'aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama nuru,” Mt 17:2. Kristo anavikwa Utukufu wake ambao ataunyakua rasmi mara baada ya mateso, kifo na ufufuko huko Yerusalemu. Hivyo Utukufu wa Kristo hautenganishwi na msalaba/mateso. Kwa maana nyingine hakuna Utukufu pasipo msalaba. Kama Kristo ndiye njia, kweli na uzima, Yoh 14:6, nasi wafuasi wake itatupasa kupita njia hiyo ya msalaba, ukweli huu anaotufundisha, ili tuufikie uzima ule, yaani maisha ya milele. Kristo ni masiha ya Msalaba, nasi twamfuata Masiha wa Msalaba ili tuifikie taji ile ya Utukufu baada ya kuhesabiwa haki.

Pili, ni ukamilifu wa nyakati. Katika tendo hili la kung’ara, tunaelezwa tokeo la watu wawili, yaani Musa na Eliya katika mazungumzano na Yesu. “Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye,” Mt 17:3. Katika tendo hili, Musa anawakilisha Torati, na Eliya Unabii. Hivyo leo Yesu anaikamilisha Torati na Unabii. Naye Yesu anatuambia, “Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza. Kwa maana, amin, nawaambia, Mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka, yodi moja wala nukta moja ya torati haitaoondoka, hata yote yatimie,” Mt 5:17-18. Torati inatimilizwa kwa amri ya upendo kwa Mungu na jirani.Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii,” Mt 7:12. Ni ndani na katika Kristo tu tunapata neema na kweli kwa mkono wake. “Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo,” Yoh 1:17. Na huku ndiko kutimilika kwa sheria na kutamalaki kwa upendo, kweli, na neema.

Leo pia unabii wote ulionenwa juu ya Kristo na historia nzima ya wokovu wetu unakamilika. Unabii huu unafika ukomo wake kwa uwepo wa Kristo ambaye ni UPENDO WA MUNGU kwetu. Mtume Paulo anasema, Upendo haupungui neno wakati wo wote; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma; yakiwapo maarifa, yatabatilika,” 1Kor 13:8. Huyu ndiye Kristo Yesu! Kung’ara kwake Bwana wetu Yesu Kristo kulikoonyesha Ufukufu wake, kunaamsha furaha ya ndani ya Mtume Petro na kuyasema ya moyoni mwake. “Petro akajibu akamwambia Yesu, Bwana, ni vizuri sisi kuwapo hapa; ukitaka, nitafanya hapa vibanda vitatu, kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya,” Mt 17:4. Hata hivyo hilo halikuwa kusudi la Yesu kubaki mlimani pale. Yesu inabidi ashuke na kuukumbatia Msalaba kama alama ya ushindi na  hapo ndipo wokovu wako na wangu ulipotundikwa. Hii ndiyo safari kuelekea kilele kile cha wokovu kama Masiha wa Msalaba.

Tatu, ni hatma yetu iliyojengeka katika agano la milele. Kristo ndiye kielelezo chetu na wokovu wetu. Leo Mungu Baba anauweka ukweli huu hadharani na kusema, “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye; msikieni yeye,” Mt 17:5. Hili ndilo agano la milele kati yetu na Mungu, na Kristo akiwa ndiye daraja na mlango halisi wa sisi kupitia kwani ni kwake tu tutakuwa salama kama njia, ni kwa Kristo tu tunalishwa kweli katika kweli, na Kristo tu ndiye uzima halisi. Hivyo hapana tena ufunuo ulio wa wazi na kamili zaidi ya ufunuo huu wa Mungu kupitia mwanaye Mpenzi. Tendo hili linathibitishwa na sauti ya Mungu mwenyewe kwa viumbe vyote, Mt 17:5. Ndugu yangu, Je, unafuata sauti gani katika maisha yako? Sauti hii kutoka mbinguni inampa Yesu Kristo Heshima, Mamlaka, na Utukufu. Maana alipata kwa Mungu Baba heshima na utukufu, hapo alipoletewa sauti iliyotoka katika utukufu mkuu, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye,” 2Pet 1:17. Nasi tunapoisikia sauti hiyo na kuishi kweli hiyo, twajazwa nguvu, heshima na utukufu kwa kuishi ndani na katika Kristo.

Wapendwa wana wa Mungu, zipo sauti nyingi katika maisha yetu. Je, sauti hizo zinatupeleka karibu na Kristo Yesu au zinatutenganisha na ukweli wake? Kusikia sauti hii ni kuyafanya mapenzi yake. Na kufanya mapenzi yake maana yake ni tuyafanye kila mmoja kadiri ya wito wake.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Wakainua macho yao, wasione mtu ila Yesu peke yake,” Mt 17:8

Tusali:-Ee Yesu, tujalie neema ya kuyafanya mapenzi yako. Amina

 

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 17 YA MWAKA-I


JUMAMOSI WIKI YA 17 YA MWAKA-I

Somo: Law 25:1, 8-17

Zab: 67:1-2, 4, 6-7

Injili: Mt 14:1-12

Nukuu:

Nawe utajihesabia Sabato saba za miaka, maana, miaka saba mara saba; zitakuwa ni siku za Sabato saba za miaka kwenu, maana miaka arobaini na kenda,” Law 25:8

“Na mwaka wa hamsini mtautakasa, na kupiga mbiu ya kuachwa mahuru katika nchi yote kwa watu wote wanayokaa; itakuwa ni yubile kwenu, nanyi kila mtu atairudia milki yake mwenyewe, nanyi mtarejea kila mtu kwa jamaa yake,” Law 25:10

“Mwaka huo wa yubile mtairudia kila mtu milki yake,” Law 25:13

“Wala msidanganyane; lakini utamcha Mungu wako; kwa kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wenu,” Law 25:17

Kwa sababu Yohana alimwambia, Si halali kwako kuwa naye,” Mt 14:4

“Hata akaahidi kwa kiapo ya kwamba atampa lo lote atakaloliomba,” Mt 14:7

“Naye mfalme akasikitika; lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya wale walioketi chakulani pamoja naye, akaamuru apewe,” Mt 14:9

TAFAKARI: “Simama katika kweli na tenda haki, mche Mungu wako kwa kuwa Yeye ndiye Bwana, Mungu wako.”

Wapendwa wana wa Mungu, ni wito kwa kila mmoja wetu na hasa aliyepewa dhamana ya kuongoza kusimama katika kweli na kutenda haki. Kufanya hivyo ni kutambua na kuongozwa na hofu ya Mungu ukijua wazi kwamba ni wajibu kiimani kumcha Mungu muumba wako kwa kuwa yeye ndiye Bwana Mungu wako. Kumcha Mungu ni kufanya yale Mungu ayapendayo na yenye kuiumba taswira yake kwa viumbe vyake. Ni kutambua kwa undani kabisa kwamba uwepo wapo bila Mungu si chochote wala lolote. Ni kutambua pia hakuna uhai bila Mungu. Hofu hii ya Mungu ndiyo kieleleza cha Ibada zote hazifanyazo mwanadamu kwa kutambua uwepo wa Mungu wake kwa kila kitu akifanyacho. Tufanyapo ibada hizi isiwe ni kutimiza wajibu tu wa kiliturjia, bali tuzame katika kweli ya kile tukifanyacho kwa Imani thabiti.

Hivyo, Waisraeli katika maana hiyo hapo juu wanaifanya sabato kuwa hai kinadharia na matendo. “Nawe utajihesabia Sabato saba za miaka, maana, miaka saba mara saba; zitakuwa ni siku za Sabato saba za miaka kwenu, maana miaka arobaini na kenda,” Law 25:8. Tendo hili linapofanyika kwa miaka 49, kilele chake, yaani mwaka ule wa 50, hufanywa yote kwa matendo zaidi. Mwaka huu ujulikana kama mwaka wa jubilee. Ni wakati wa kuanza upya katika yote, kusamehe yote, kuachilia yote, na hasa wafungwa. Kwa ujumla ni mwaka wa kuishi kimatendo upendo wa Mungu. Mwaka huo wa yubile mtairudia kila mtu milki yake,” Law 25:13

Ni mwaka wa kuishi neema na baraka za Mungu. Kila mmoja alitafuta namna ya pekee kabisa kujitakasa na kuwa mpya mwili na roho. Hivyo, “mwaka wa hamsini mtautakasa, na kupiga mbiu ya kuachwa mahuru katika nchi yote kwa watu wote wanayokaa; itakuwa ni yubile kwenu, nanyi kila mtu atairudia milki yake mwenyewe, nanyi mtarejea kila mtu kwa jamaa yake,” Law 25:10. Hakika ni kipindi cha upatanisho wa kweli na kuishi katika haki na kweli ya Mungu. Hii ndiyo hofu ya Mungu itusukumayo kumcha usiku na mchana. Naye Mungu anasema, “wala msidanganyane; lakini utamcha Mungu wako; kwa kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wenu,” Law 25:17

Mpendwa, katika Injili ya leo tunaona hathari za matumizi mabaya ya madaraka yanayosababisha maafa makubwa kwa wale watetezi wa haki katika jamii inayowazunguka. Ni jambo la hatari sana kuwa na kiongozi anayeongozwa na mihehuko ya hisia zake, huku akitegemea sifa kutoka kwa watu. Kiongozi mwenye misukumo hii ya kihisia ni rahisi sana kuzikanyaga haki za wale anaowaongoza. Hii ni pamoja na kuwa makini katika ahadi azitoazo kiongozi mbele za watu. Herode anamwahidia binti yake chochote apendacho baada ya kucheza vizuri na kuufurahisha umati wa watu siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwake. Hata akaahidi kwa kiapo ya kwamba atampa lo lote atakaloliomba,” Mt 14:7. Mfalme Herode anajifunga kwa kauli yake mwenyewe. Mfalme Herode hakuwa na lakusema binti yake alipokitaka kichwa na Yohane Mbatizaji zaidi ya kutimiza ahadi yake na kulinda heshima yake kama kiongozi. Naye mfalme akasikitika; lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya wale walioketi chakulani pamoja naye, akaamuru apewe,” Mt 14:9. Je, ni watu wangapi huwa kafara kunakotokana na utafutaji wa sifa na umaarufu wa baadhi ya viongozi wetu?

Ni mbaya sana kutafuta umaarufu kwa kukanyaka haki za watu, na hasa wale ambao wapo kinyume chetu kutokana na matendo yetu yasiyo haki na hofu ya Mungu. Yohane Mbatizaji ni mhanga wa viongozi wale wenye kupenda sifa na umaarufu. Kosa la Yohane Mbatizaji ni kusimama katika kweli. Umauti unamfika Yohone Mbatizaji kwa sababu alimwambi Mfalme Herode Si halali kwako kuwa naye,” Mt 14:4. Wapo wahanga wengi wa mtindo wa Yohane Mbatizaji katika familia zetu, Jumuiya zetu ndogondogo za Kikristo, Jumuiya zetu za kitawa, Makanisani mwetu, sehemu zetu za kazi, na mbaya zaidi leo katika mfumo mzima wa utawala. Wapendwa tuutafute kwanza ufalme wa Mbinguni na mengine yote tutapewa kwa ziada.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Hata akaahidi kwa kiapo ya kwamba atampa lo lote atakaloliomba,” Mt 14:7

Tusali: Ee Yesu tujalie imani thabiti tuutafute ufalme wa mbingni. Amina